Benki ya KCB imetenga shilingi bilioni 250 aitakazotumika kuwafadhili wanawake wawekezaji katika kipindi cha miaka 5 ijayo.
Ufadhili huo unaolenga biashara zinazomilikiwa na kusimamiwa na wanawake kote nchini unalenga kuimarisha mchango wa benki hiyo katika ukuaji wa uchumi.
Ili kuafikia mpango huo KCB tayari imerahisisha matakwa na stakabadhi zinazohitajika ili kuharakisha mipango ya kutoa mikopo. Pia wanawae hao wawekezaji wataweza kupokea usaidizi usio wa kifedha kutoka mashirika mbalimbali yanayoshirikiana na benki hiyo.
Pia biashara hiyo zinatarajiwa kunufaika kwa kupatikana kwa masoko ya bidhaa na huduma zake kando na kubuni nafasi za kazi.
Fedha hizo zitatolewa kwa awamu; shilingi bilioni 50 kwa mwaka.
Afisa Mkuu Mtendaji wa KCB Paul Russo anasema kitengo hicho cha biashara kina nafasi nzuri katika kuchangia ukuaji wa uchumi si tu humu nchini bali Afrika Mashariki.
Russo amesema watafanya mazungumzo na wanawake hao ili kuwashauri namna ya kukabili changamoto za kibiashara ili kuimarisha mapato yao.
Miongoni mwa changamoto alizozitaja ni ukosefu wa ufadhili wa kifedha, kutojumuishwa katika nafasi za kufanya maamuzi na changamoto za kijamii na hata kisheria.Takwimu zinaonesha kwamba asilimia 80 ya biashara zinazomilikiwa na wanawake hukosa ufadhili wa kifedha kama vile kupata mikopo, ukosefu au kabadhi muhimu zinazohitajika.
Amesema Benki hiyo imejitolewa kuwajumuisha wanawake katika kuafikia Malengo ya Maendeleo ya Kimataifa hasa kuhusu kukabili umasiki, mazingira mazuri ya kufanyia kazi, Ukuaji wa uchumi na kupunguza ukosefu wa usawa.
Masuala yatakayofanywa kipau mbele na benki hiyo ni kuongeza thamani ya mikopo wanayopewa wanawake hasa kwa kuyalenga makundi maalum kama vile walemavu.
Inatarajiwa mpango huu utachangia pakubwa katika kubuni masoko ya kimataifa yatakayosaidia uwekezaji wa wanawake si tu humu nchini bali pia kimataifa.