Maafisa wa Idara ya Upelelezi DCI katika Kaunti ya Kiambu wanachunguza kisa cha kushangaza ambapo msichana wa miaka 15 anadaiwa kuwaua ndugu zake watatu, pamoja na binamu yake katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita.
Inaarifiwa kwamba msichana huyo ambaye ni mwanafunzi wa kidato cha kwanza, amekiri kutekeleza mauaji hayo katika kituo cha Polisi cha Kikuyu, ambako anaendelea kuzuiliwa huku uchunguzi ukiendelea.
Taarifa ya polisi inasema baba wa msichana huyo alijiwasilisha katika Kituo cha Polisi cha Kikuyu akiwa amechanganyikiwa baada ya kumshuku mwanawe kwa tuhuma za mauaji.
Baba huyo aliandikisha ripoti dhidi ya msichana huyo wa umri wa miaka 15, akimshuku kwa madai ya kuwaua ndugu zake watatu, madai ambayo msichana mwenyewe amekiri kutekeleza katika tarehe tofauti tofauti.