Jumla ya kesi 9 zimewasilishwa kuhusu matokeo ya kura ya Urais ambapo William Ruto alitangazwa na Mwenyekiti wa IEBC Wafula Chebukati kuwa mshindi.
Kesi hizo ziliwasilishwa Jumatatu kabla ya makataa ya siku 7 ya kuwasilishwa kukamilika.
Katika ratiba ya mahakama, hatua inayofuatia ni kuwasilishwa kwa stakabadhi za kesi kwa washtakiwa, shughuli ambayo inafaa kufanyika Jumanne.
Kisha kutakuwa na siku 4 za walioshtakiwa kujibu kufikia Jumamosi yaani tarehe 27 Agosti.
Jumapili, walalamishi watakuwa na siku nyingine 1 kuwajibu washtakiwa.
Kisha kwa siku nyingine 2, pande zinazohusika zitakuwa huru kuomba maamuzi mbalimbali kwa ajili ya kesi hiyo kufanywa yakiwamo maombi ya kuwasilishwa kwa stakabadhi mbalimbali yaani Interlocutory application.
Kikao cha kuratibu vikao, Pre-Trial Conference kinatarajiwa kufanyika Jumanne wiki ijayo. Jumatano wiki ijayo marafiki wa mahakama, Amicus Curiae watakuwa na nafasi ya kuwasilisha hoja zao kabla ya pande zote kuanza kumenyana katika Mahakama ya Juu.
Uaumuzi unatarajiwa kutolewa tarehe 5 mwezi Septemba.