Na, Sophia Chinyezi
Benki Kuu Nchini CBK imetoa makataa ya wiki mbili kwa benki zote kuanza kutekeleza sheria ya marekebisho ya benki iliyotiwa saini na Rais Uhuru Kenyatta wiki mbili zilizopita. Kwenye taarifa kwa benki hizo, CBK imeonya kwamba benki ambazo zitaendelea kuwatoza wateja wao riba zaidi ya kiwango kilichowekwa zitaadhibiwa. Imesema benki ambazo hazitatii sheria hiyo mpya zitatozwa faini ya shilingi milioni moja au mkurugenzi mkuu wa benki zinazohusika kuhukumiwa kifungo cha mwaka mmoja gerezani. Agizo hilo linajiri huku benki ya Co-operative ikitangaza kwamba itapunguza viwango vya riba kwa wateja wake waliochukua mikopo awali. Ikumbukwe Ijumaa iliyopita benki hiyo ilikuwa ya kwanza kutangaza kwamba itatekeleza sheria hiyo, ingawa kwa wanaochukua mikopo baada ya sheria hiyo kupitishwa. Kufikia sasa ni benki nne pekee ndizo zimetangaza kupunguza viwango vya riba.