Na, Carren Omae
Vita dhidi ya ufisadi vinatatizwa na sheria zisizo na makali, ukosefu wa nia njema kutoka kwa walio mamlakani na mivutano ya ubabe katika Tume ya Maadili na Kukabili Ufisadi, EACC. Kauli hii imetolewa na Mwenyekiti wa Tume ya Utawala wa Haki, Otiende Amollo. Kwa mujibu wa Omollo, ufisadi unaendeleza ukosefu wa haki mahakamani na wahusika kuepuka adhabu. Akihutubu mjini Mombasa wakati wa mkutano wa kila mwaka wa Chama cha Wanasheria Nchini LSK, Mwenyekiti huyo amesema, Kenya haijaweka mikakati ya kutosha kupiga vita ufisadi. Wakati uo huo, amesema EACC ilivyobuniwa, haina makali ya kukabili uovu huo, huku akisema kubadilishwa kwa sheria kila mara na uchunguzi unaochukua muda mrefu, ni mambo yanayolemaza vita dhidi ya ufisadi. Aidha, amelilaumu bunge kwa kutotekeleza majukumu yake kikamilifu wakati wa kuwakagua maafisa wa umma.