Serikali imesisitiza kwamba haitaruhusu adhabu ya vibiko dhidi ya wanafunzi katika shule za humu nchini. Waziri wa Elimu Profesa George Magoha amesema haifai walimu kuwashurutisha wanafunzi kupata alama za juu katika mitihani.
Akizungumza katika Shule ya Msingi ya Wagwer Kaunti ya Siaya, Waziri Magoha amesema mwalimu anayesemekana kumwadhibu kwa kumchapa mwanafunzi katika Shule ya Msingi ya Nyamninia atachukuliwa hatua. Magoha amesema maafisa wa polisi na wale wa Tume ya Huduma za Walimu TSC wanashirikiana katika uchunguzi huo.
Mwalimu huyo alikamatwa jana na anatarajiwa kufikishwa mahakamani Jumatatu.
Ikumbukwe japo walimu wanaruhusiwa kuwaadhibu wanafunzi sehemu ya 29 ya katiba imepiga marufuku adhabu ya viboko shuleni.
Wakati uo huo, Magoha amewaonya walimu dhidi ya kuwahangaisha wanafunzi kwa kutotimiza mahitaji mbalimbali yakiwemo malipo ya masomo ya ziada akisema serikali kupitia wizara ya elimu wamewekeza vilivyo kwa wanafunzi hao na hivyo hawafai kutumiwa nyumbani kwa sababu ya pesa.
Kuhusu ujenzi wa madarasa ili kufanikisha mpango wa mtaa wa umilisi Magoha amesema ujenzi wa madarasa yote 3, 500 unatarajiwa kukamilika mwezi Agosti.