Rais Uhuru Kenyatta ametangaza rasmi kupunguzwa kwa bei za unga wa mahindi ambapo pakiti moja ya kilo mbili, itauzwa kwa kati ya shilingi mia moja na mia moja na tano nchini kote.
Agizo la Rais limetolewa kufuatia malalamishi ya wananachi kutokana na kupanda kwa ghama za maisha, ambapo pakiti moja ya kilo mbili za unga imekuwa ikiuzwa shilingi zaidi ya mia mbili na tano.
Katika hotuba yake akiwa Ikulu ya Nairobi, Rais Kenyatta ametangaza kwamba serikali imeondoa ushuru na kodi ya ziada kwenye mahindi yanayoagizwa kutoka nje ya Kenya, kama njia mojawapo ya kupunguza gharama za maisha.
Wakati uo huo, rais amekiri kwamba taifa la Kenya linakumbwa na changamoto za kiuchumi, na kueleza haja ya washikadau mbalimbali kushirikiana na serikali katika kuwakwamua wananchi kiuchumi.
Rais ametumia fursa hiyo kukashifu mrengo wa Naibu wa Rais William Ruto, akisema ni unafiki kwa viongozi waliopo mamlakani kuwa wa kwanza kulalamika kuhusu bei za unga wa mahindi badala ya kutafuta suluhu.
Mrengo wa Ruto umekuwa ukiishutumu serikali kwa madai ya kushindwa kudhibiti uchumi wa nchi, na kudai kwamba inatumia kipindi hiki cha uchaguzi kuwahadaa wananchi kwa kupunguza bei ya unga.