Kikao cha kwanza cha Mahakama ya Juu ambacho ni cha kuratibu jinsi kesi za kupinga uchaguzi wa urais zitakavyosikilizwa kitafanyika Jumatatu hii katika Mahakama ya Milimani, Nairobi.
Notisi iliyotolewa na Msajili wa Mahakama ya Juu L.M Wachira, inaonesha kwamba kikao hicho kitaanza saa tano asubuhi.
Masuala makuu katika vikao hivyo ni kujumlisha masuala katika kesi zote tisa, kuamua muda utakaotumika katika kesi na jinsi ratiba kamili itakavyokuwa.
Kwa mujibu wa Msajili Mkuu wa Mahakama Anne Amadi, idadi ya juu zaidi ya mawakili watakaoruhusiwa kuwawakilisha walalamishi na washtakiwa ni 4 japo huenda mabadiliko yakafanywa kutegemea na kikao cha Jumatatu.
Majaji wote saba wa Mahakama ya Juu watashiriki kesi tofauti na mwaka 2017 wakati ambapo walikuwa sita tu. Majaji hao ni Jaji Mkuu Martha Koome, Naibu Jaji Mkuu Philomena Mwilu, Majaji Smokin Wanjala, William Ouko, Mohamed Ibrahim, Isaac Lenaola na Njoki Ndung'u.
Kadhalika kutakuwa na majaji waangalizi 11 wakiongozwa na aliyekuwa Jaji Mkuu nchini Tanzania Mohamed Othman.
Ikumbukwe tofauti na awali ambapo vikao hivyo vilifanyika katika majengo ya Mahakama ya Juu, wakati huu vinafanyika eneo la Milimani ili kukidhi mahitahi ya wanaotarajiwa kuwa vikaoni.