Bunge la Seneti limebuni kamati ya kutatua mzozo kati ya Joho na Bunge la Kaunti

Bunge la Seneti limebuni kamati ya kutatua mzozo wa kisiasa kati ya Gavana wa Mombasa Ali Hassan Joho na wawakilisha wadi wa bunge la Mombasa. Mzozo huo ambao ulianza wakati gavana Joho alitishia kuanzisha mchakato wa kuwatimua  baadhi ya wawakilishi  kwa madai ya kukosoa utendakazi wake, sasa umefika mbele ya kamati za ugatuzi na maendeleo ya serikali.

Joho ambaye anatarajiwa leo hii kufika mbele ya kamati hiyo chini ya uenyekiti wa Seneta wa Laikipia John Kinyua, anatarajiwa kuweka wazi chanzo cha mgogoro baina yake na wawakilisha hao.  Licha ya shughuli za maridhiano kuendelea, kiongozi huyo ameapa kuendelea na kushinikiza kutimuliwa kwa baadhi ya wawakilisha anaowataja kuwa waasi na maadui wa maendeleo.

Kwa upande mwingine, Joho amelaumiwa na wawakilishi hao kwa kuzembea na kutelekeza majukumu yake akiwa gavana, suala ambalo amepuuzilia mbali akilitaja ni njama ya kumlenga visisyo. Kamati hiyo vilevile  imemualika spika wa bunge la Mombasa Aharub Khatri, kutoa mwanga zaidi kuhusu mzozo huo ambao umetishia kusambaratisha huduma za maendeleo  kwenye kaunti ya Mombasa.

Kulingana na katiba ya taifa kipengele cha 104, wapiga kura tu ndio wenye uwezo wa kumnga'atua mamlakani  mbunge  yeyote kabla ya kukamilika kwa muda wake uongozi. Kadhalika inasema kwamba bunge litaanzisha shughuli ya kuchunguza madai yanayolengwa  kabla ya kutimuliwa kwa kiongozi yeyote. Gavana Joho amesema atazindua shughuli  ya kukusanya saini ya wakazi kuwatimua wawakilishi  hao uongozini.

Ikiumbukwe kwamba magavana wote  47,  wamekuwa katika mzozo wa kila mara  na wawakilishi wa wadi kuhusu matumizi ya fedha kwenye kaunti mbalimbali

Related Topics