Wakuu wa Polisi wahamishwa kwenye mabadiliko ya hivi punde

Siku chache baada ya kuidhinishwa rasmi kuwa Naibu Inspekta Mkuu wa Polisi, Joel Kitili amefanya mabadiliko katika idara ya polisi kwa kuwahamisha baadhi ya wakuu wa polisi hadi kaunti nyingine. Caren Omae na taarifa zaidi.
Kwenye mabadiliko hayo, aliyekuwa Msemaji wa Polisi Zipporah Mboroki amepewa uhamisho hadi eneo la Lari, wadhifa wa OCPD.  Mkuu wa Polisi Buruburu, Richard Kerich ndiye Naibu Kamanda mpya Kaunti ya Nairobi. Aliyekuwa Kamanda wa Trafiki eneo la Bonde la Ufa Mary Wangui Omari amehamishwa hadi Tharaka-Nithi kuwa Kamanda wa Kaunti.
Aidha aliyekuwa OCPD wa Masaba Kaskazini, Patterson Maelo ameteuliwa kuwa Kamanda wa Polisi Kaunti ya Mombasa huku Kipkemboi Rop akiwa Kamanda wa Taita Taveta. Aliyekuwa Kamanda wa Trafiki eneo la Nyanza, Joshua Omukata ndiye OCPD mpya wa Nakuru.
Mmoja wa wakuu wa walinzi wa Naibu wa Rais, Surpritendent Noah Maiyo amepewa uhamisho hadi kitengo cha ulinzi wa Rais katika Ikulu. Kwa ujumla maafisa watano wameteuliwa kuwa makamanda huku wengine hamsini na tisa wakihamishwa hadi maeneo mbalimbali nchini. Hivi majuzi, Tume ya Huduma kwa Polisi NPSC ilisema baadhi ya maafisa wa polisi waliofanyiwa mchujo watapandishwa vyeo.
Na, Beatrice Maganga

Related Topics

Police transfers