Mgombea wa urais wa UDA William Ruto yuko katika Kaunti ya Narok ambapo anaendeleza kampeni za Kenya Kwanza kupigia debe azma yake kuwa urais.
Ruto ameandamana na vigogo wa Kenya Kwanza Musalia Mudavadi, mwenzake wa FordKenya Moses Wetangula miongoni mwa wengine.
Akizungumza katika eneo la Kilgoris, Ruto ameahidi kuwa uongozi wake utashughulikia matatizo ambayo yamekuwa yakiwakumba watu wa Jamii ya Maa kwa muda na kuwataka kumuunga mkono Agosti tisa.
Wandani wake Moses Wetangula, Musalia Mudavadi na Ndindi Nyoro wameendelea kumpigia debe Ruto wakisema kwamba anauwezo mkubwa wa kufanikisha mabadiliko ya uongozi nchini na kuitaka Jamii ya Maa kumuunga mkono.
Aidha wamemtaka Rais Uhuru Kenyatta kukoma kujihusisha na siasa za urithi na badala yake kuwaachia Wakenya nafasi ya kumchagua kiongozi wao.
Ruto baadaye Alasiri ya leo atazuru Kiambu kupigia debe azma yake wakati ambapo mvutano unaendelea kutokota miongoni mwa wa wagombea wa ugavana wa Kiambu wanaohisi kuwa Ruto anampendelea Kimani wa Matangi wa UDA.
Tayari Moses Kuria na William Kabogo wametishiakutohudhuria mikutano ya kumpigia debe Ruto wakitaka ashughulikie malalamiko yao.