Kinara wa Chama cha Azimio Raila Odinga amelalamikia vikali kuzuiwa kwa wanahabari kufuatilia moja kwa moja uchunguzi na ufukuzi wa mili unaofanyika kwenye eneo la Shakahola katika Kaunti ya Kilifi.
Akizungumza kwenye eneo la Kibra muda mfupi baada ya kurejea nchini kutoka Dubai, Raila amekitaja kisa cha Shakahola kuwa kisa ambacho kinahitaji kuangaziwa zaidi kwani hakijawahi kushuhudiwa katika historia.
Raila vilevile ametumia fursa hiyo kuzua kumbukumbu za wakati mkewe Ida Odinga alishauri sekta ya dini kuwa na mpangilio akisema sasa imedhihirika wazi alichokuwa akimaanisha.
Wakati uo huo, Raila Odinga sasa ametangaza rasmi kwamba maandamano yatarejelewa rasmi siku Jumanne.
Kuhusu mazungumzo amesisitiza kwamba mrengo wake hautalegeza msimamo wa kumtaka Mbunge wa Eldas Adann Keynan aondolewe katika kamati ya mazungumzo baina ya serikali na upinzani.
Raila vilevile amesisitiza kwamba Mbunge wa Pokot Kusini Davdi Pkosing yuko huru kusalia katika kamati hiyo licha ya Chama cha KUP kusaini mkataba na UDA.
Raila ametumia fursa hiyo kuendelea kuwasuta polisi kwa kumkabili yeye na wafuasi wake wakati wa maandamano yaliyositishwa.