Na, Sophia Chinyezi
Wabunge wa eneo la Pwani wamesema hawajanunuliwa kujiunga na muungano wa Jubilee, bali wanafanya hivyo kwa kutaka kulingana na maendeleo wanayoona katika maeneo bunge wanayowakilisha. Wabunge hao Gideon Mungaro, Mustafa Iddi, Harrison Kombe, Masoud Mwahima , William Kamoti, Mshenga Mvita, Emma Mbura na Mwakilishi wa Kike Zainab Chidzuga. Chidzuga amewataka wananchi wa Pwani kuiunga mkono Jubilee kwa manufaa ya maendeleo. Kwa upande wake Mung'aro amesema raia wa eneo hilo hawatatumiwa kwa manufaa ya watu binafsi huku wakiangamia katika umaskini. Kadhalika amesema viongozi wengi wa Pwani wanashirikiana na serikali na kuwataka wananchi kutopotoshwa. Naibu wa Rais William Ruto amewaomba wakazi wa Pwani kujiunga na Jubilee Party kwa kuwa ina agenda bora ya maendeleo. Ruto amewahakikishia walio katika chama hicho kwamba watafanya uteuzi kwa njia huru na haki. Ameitaka Serikali ya Kaunti ya Kilifi kutumia vyema shilingi bilioni 9.6 kuboresha viwanda vya eneo hilo ambavyo vitawanufaisha wakazi wa kaunti hiyo. Wakati uo huo amesisitiza kwamba serilkali ya Jubilee itawahudumia Wakenya kwa usawa bila kujali kabila, imani, eneo wanalotoka wala vyama wanavyounga mkono. Wameyasema hayo katika uwanja wa Shule yaSekondari ya Krapf Memorial ambapo Naibu wa Rais William Ruto alitoa hati miliki katika eneo la Rabai Kaunti ya Kilifi.