Aukot aitaka serikali kuwachukulia hatua polisi wanaotumia nguvu kupita kiasi

Kiongozi wa chama cha Thirdway Alliance Dakta Ekuru Aukot sasa anaitaka serikali kuwachukulia hatua za kisheria maafisa wa polisi watakaopatikana wakitumia nguvu kupita kisasi wakati wa kutekeleza agizo la kutopatikana nje.

Kwa mujibu wa Aukot, maafisa wa usalama walionakiliwa kwenye kanda za video wakiwapiga na hata kuwajeruhi waliokiuka agizo hilo la Rais Uhuru Kenyatta wanapaswa kutambuliwa na kuadhibiwa na kuitaka Idara ya Upelelezi, DCI kufanya uchunguzi wa kina kuhusu visa hivyo.

Wakati uo huo, kupitia barua kwa Inspekta Mkuu wa Polisi Hillary Mutyambai, kiongozi huyo ametoa wito kwa Rais Uhuru Kenyatta kubatilisha muda wa kutekelezwa kwa agizo hilo kutoka saa moja usiku hadi saa tatu usiku ili baadhi ya familia ziweze kukidhi mahitaji ya familia zao.

Kauli yake inajiri siku chache tu baada ya maafisa wa usalama kutumia nguvu kupita kiasi kudhibiti watu waliokuwa katika kivuko cha Likoni Feri, jijini Mombasa.

Katika tukio hilo, Shirika la Msalaba Mwekundu RedCross lilithibitisha kuwa takribani watu hamsini walijeruhiwa miongoni mwao ajuza mmoja ambaye alipata majeraha kwenye mgongo wake.

Aidha viongozi katika Kaunti ya Mombasa wakiongozwa na Mbunge wa Mvita Abdulshwamard Shariff Nassir waliikosoa vikali hatua hiyo na kuitaka serikali kuongeza muda wa amri ya kutopatikana nje kuanzia saa mbili usiku hadi saa kumi na moja alfajiri badala ya kuanzia saa moja usiku.