Msako mkali kuanzishwa na maafisa wa TSC dhidi ya walimu

Msako mkali unatarajiwa kuanzishwa asubuhi hii na maafisa wa Tume ya Huduma za Walimu, TSC dhidi ya walimu ambao hawajasajiliwa rasmi na tume hiyo lakini wanafunza katika shule za umma na za binafsi.

Msako huo unawalenga walimu ambao waliondolewa katika orodha ya TSC kwa sababu za nidhamu zikiwamo dhulma za ngono na wakarejea kufunza kwa kutumia njia za mkato.

Ili kufanikisha shughuli hiyo, TSC inashirikiana na maafisa wa Wizara ya Elimu ambao watachangia kutathmini na kuwatambua walimu ambao wanaendesha shughuli zao kinyume na sheria huku ikibainika kwamba baadhi ya shule zimekuwa zikiwaajiri wanafunzi waliokamilisha kidato cha nne.

Ikumbukwe kwamba kwa mujibu wa sheria za TSC, yeyote anayejihusisha na masuala ya uwalimu sharti awe amesajiliwa rasmi kuwa mwalimu baada ya kuhitimu mafunzo.

Kwa mujibu wa ripoti iliyowasilishwa bungeni mwezi Machi mwaka huu, TSC ilidokeza kwamba walimu elfu moja, mia mbili ishirini na wanane walitimuliwa katika kipindi cha miaka saba iliyopita kwa kuhusishwa na visa vya mapenzi na walimu.