Raila amwaga hasira kwa Orengo na Sifuna baada ya matokeo duni kwenye uchaguzi

Kiongozi wa wachache katika bunge la Seneti James Orengo na kiongozi wa ODM Raila Odinga katika mkutano wa siasa ya zamani. [Picha: Standard]

Ama kwa kweli mambo yanayoendelea ndani ya nyumba za watu unaweza kupigwa na butwaa kusikia haswa nini kinachoendelea kila kukicha. Baadhi ya viongozi wa chama maarufu cha ODM ambao daima wamemkiria kinara wake wa kitaifa Raila Odinga “Baba” kuwa kuwa ni simba aliyenyeshewa na mvua baada ya mkono wake wa buheri na Rais Uhuru Kenyatta, walipigwa na mshangao wakati alipowakemea miongoni mwa viongozi wake ambao huropokwa maneno bila kupima uzito wake.

Kulingana na mkaribu wa afisi za Orange House, makao makuu ya chama na wale ambao walihudhuria kikao cha ghafla katika afisi za Raila maeneo ya Capital Hill majuma mawili yaliyopita, walitokwa na jasho la miguuni kufuatia kikarango cha msomo alichowapasha Seneta wa Siaya, James Orengo na Edwin Sifuna, katibu mkuu wa chama cha ODM. Chanzo cha msomo ni nini? Kulingana na habari za ndani zatueleza kuwa Baba aliwafokea Orengo na Sifuna kuwaelezea kutoridhika kwake na matokeo ya uchaguzi mdogo wa Ugenya na ule wa Embakasi ambapo ODM ilinoa patupu viti vyote hivi.

Isitoshe, yasikika kwamba alimwambia Orengo afunge domo lake la tepwe vile vile Edwin Sifuna ambaye anatajwa kama katibu wa kwanza wa chama mwenye mori wa kutaka kutoa taarifa za chama bila kupata mwelekeo maalum kutoka kinara wao.

Ujasusi wa Wajir Suala lingine ambalo lilijitokeza kwenye kikao hicho cha dharura, ni kutokuwa na habari za ndani za kijasusi kuhusiana na jinsi mporomoko wa chama ulivyoendelea katika maandalizi ya uchaguzi mdogo wa Wajir. Mwakilishi aliyekuwa katika mstari wa mbele kuwania kiti hicho kwa tikiti ya ODM Mohamed Yusuf, alitongozwa na adui mkubwa wa chama, Naibu wa rais William Ruto na kubumburusha matumaini ya ODM ya Wajir baada ya kurambishwa mchanga Ugenya na Embakasi.

Baba, aliyekuwa na hasira lakini za wastani kwa kuwa ni mtu mzima ni kiongozi wa wote wawe wabaya ama wazuri, yasemekana hakusita kuregelea suala la jinsi kesi ya nidhamu baina ya wabunge wawili wa Pwani, Aisha Jumwa (mbunge wa Malindi) na mwenzake Suleiman Dori (Msambweni) ilivyopelekwa na usimamizi wa chama. Habari za mashinani kutoka pwani, Raila aliwaambia kamwe siyo za kuridhisha hata kidogo hususani sifa na hadi ya chama inavyodorora katika eneo bunge la Msambweni ambako licha ya mbunge Suleiman Dori kusamehewa na chama, ni kana kwamba amepunguzia umaarufu chama zaidi ya sifa. Hapo, alionyesha ulegevu wa Sifuna na kumtaka kupiga msasa mbinu zake za kukabiliana na masuala sawa kama hayo siku za usoni.

Mswada wa Ruto Baada ya kumkabili katibu wake wa chama, alirejea kwa rafiki yake seneta wa Siaya, James Orengo ambaye alimwabia kinaga ubaga kwamba kadiri anavyozidi kumkashifu naibu rais William Ruto ndivyo anavyozidi kumtafutia sifa adui. Kwa mfano, alimwambia tabia alizoonyesha wakati wa kampeini za Ugenya na Emabakasi za kumtaja Ruto ni kana kwamba anashindana naye, ziliwaponza.

“Achana kabisa na kuimba jina ya huyu mtu. Wacha mambo ya kuzungumzia mswada wa kumkabili bungeni, wacha kufananisha huyu mtu na kitu chochote cha chama, huyu siyo wa ligi yangu utampatia sifa za bure,” yadaiwa ni mfano wa maneno ambayo Baba alimuonya Orengo juu ya Ruto.

Hii inafuata baada ya chama cha ODM na viongozi wake kuaibika pakubwa kufuatia matokeo ya uchaguzi mdogo wa Ugenya na Embakasi ikisemekana kwamba vinara walioachiwa majukumu na Raila kuendesha kampeini za ODM, walimkampenia Ruto kuliko wagombea wao kutokana na kuimba kwamba watakapomchagua mpinzani wao, watakuwa wamempatia ushindi Ruto.

Ni kikao hichi ambapo pia kiongozi wachama alimwamuru mwenyekiti John Mbadi kuhakikisha kwamba hakuna taarifa za kiholela zitakazotolewa bila ya maafikiano maalum baina ya uongozi wa chama na usimamizi wa afisi. Hii inadhiri baada ya kupata habari kwamba katibu wake amekuwa akizuru hususani pwani na sehemu nyinginezo na kukejeli wafuasi wa wabunge wakinzani bila ya utaratibu wowote. Kwa mfano yasemekana alizuru katika kaunti ya Kilifi na kuanza kuzurura na aliyekuwa mbunge wa Malindi, Willy Mtengo akimwahidi kwamba atakuwa mgombea wa chama wakati uchaguzi mdogo utaitishwa endapo rufani ya Aisha Jumwa itatupwa na afisi ya msajili wa vyama.

Hapa Raila yadaiwa alimsomea kwamba uamuzi wa nani atawania kwa tikiti utafanywa na mchujo wa wanachama wenyewe wa Malindi lakini siyo uamuzi wa mtu binafsi. Katika siasa ya chama pia kumezuka changamoto kwamba wengine wanamtaka katibu Edwin Sifuna atimuliwe huku baadhi yao wakisema apewe muda ajirekebishe kama mwanaadamu ambaye kila mmoja hayuko kamili.