Rais Uhuru Kenyatta, akiandamana na Mkewe Bi Margaret Kenyatta, wameratibiwa kuongoza taifa kuutazama mwili wa Hayati Rais Mstaafu Mwai Kibaki kuanzia saa nne asubuhi Jumatatu katika Majengo ya Bunge.
Kwa mujibu wa Kamati ya Kitaifa ya Mazishi iliyopewa jukumu la kupanga mipango ya mazishi, Kenyatta atawasili katika Majengo ya Bunge saa nne kamili ili kuutizama mwili wa Kibaki.
Viongozi wa Serikali ambao kuhudhuria kwao kunahitajika kwa sababu za itifaki tayari wamejulishwa, ambapo walitakiwa kuwa katika majengo ya bunge kufikia saa tatu .
Waliowasili mapema ni Jaji Mkuu Martha Koome, Spika wa Bunge la Kitaifa Justin Muturi na mwenzake wa Seneti Ken Lusaka. Naibu wa Rais William Ruto atawasili na mkewe kabla ya Rais Kenyatta kufika.
Vikosi vyote vya Maafisa wa Jeshi la Ulinzi wa Kenya KDF vipo katika majengo ya bunge kuendesha shughuli hiyo ambayo ni ya kijeshi ikizingatiwa kwamba Kibaki alikuwa amiri jeshi mkuu alipokuwa rais tangu mwaka wa 2002 hadi 2012.