Na, Carren Omae
Ikiwa imesalia miezi kumi na mwili tu kabla ya uchaguzi mkuu ujao, Rais Uhuru Kenyatta amefanya mkutano na Magavana leo hii kujadili utayarifu wao kuhusu usalama wakati wa shughuli hiyo. Mkutano huo umeandaliwa faraghani katika Ikulu ya Nairobi na kuhudhuriwa na Magavana 11. Akihutubu baada ya mkutano huo Mwenyekiti wa Baraza la Magavana Peter Munya amesema serikali za kaunti zitashirikiana na serikali kuu katika kuafikia majukumu ya Mamlaka ya Usalama katika Kaunti, County Policing Authority, vile vile kukabili matamshi ya uchochezi wakati wa kampeni na uchaguzi mkuu ujao. Aidha kwenye kikao hicho wameafikiana kwamba mamlaka hiyo itakuwa inatoa taarifa kuhusu usalama wa kaunti kila baada ya wiki mbili. Wakati uo huo, amesema Wakenya wote waliotimia umri wa miaka kumi na minane na zaidi watapewa vitambulisho vya kitaifa ili kuwawezesha kushiriki uchaguzi huo. Miongoni mwa waliohudhuria mkutano huo ni Mwenyekiti wa Baraza la Magavana ambaye pia ni Gavana wa Meru Peter Munya, Evans Kidero wa Nairobi, Kivutha Kibwana wa Makueni na Jack Ranguma wa Kisumu.