Je, bara Afrika itapata hadhi yake dunia ya leo

Bara la Afrika limekuwa na chanagmoto sufufu katika ulimwengu wa sasa hususan kutengwa katika maswala nyeti ya walimwengu. Mataifa ya Ulaya na mshirika wake mkuu wa Marekani wamejibandika ukuu wa wanadamu bila ya idhini ya washika dau husika. Mkuu wa tawi la chuo kikuu cha Moi mkoa wa Pwani Daktari Mbwarali Kame anaamini kwamba Afrika imenyimwa mgao wake wa haki katika sekta zote.

‘Wazungu wamewanyima wafrika haki kwa kuwagandamiza na kuwabagua katika maamuzi ya wote’ asema Kame na kuongeza kuwa Umoja wa Mataifa ni jukwaa danganyifu la kuwapandikisha wazungu na kuwashusha hadhi wafrika. Twaweza kukubaliana na maoni ya Kame kwa misingi ya matukio yanayoendelea katika ulimwengu wa sasa ya mwenye nguvu mpishe.

 Mataifa tajiri ya kizugu yameanzisha makundi na asasi zao za kupanga mbinu za kufaidika na kuwazuia wafrika kufaidika. Leo hii kuna jumuiya za wakubwa ama mabwenyenye kama G-5 ma G-20 zenye kudhibiti chumi za dunia.

Haya ni mataifa yaliyo na uchumi wa hali ya juu. Katika Umoja wa Mataifa ndio kuna unafiki wa hali ya juu. Ingawa falsafa ya umoja huu ni usawa wa mataifa yote wanachama lakini wanaodhibiti maamuzi nyeti ni mataifa ya kizungu. Aidha kila nchi mwanachama ana kura moja lakini pia  kundi la mataifa matano limewekwa kisheria kuzima maamuzi ya wengi.

Kikundi hichi cha nchi tano kina kura ya turufu yaani ‘veto power’ ambapo kwayo nchi moja ya hizi yaweza kuzima maamuzi ya wanachama wote kwa kukataa tu! Uwezo mkuu Nchi hizi tano za kura turufu ni Marekani, Uingereza, Uchina, Ufaransa na Urusi. Mfano mmoja ni kwa Marekani kutumia kura hii kukinga kipenzi chake, taifa la Israeli kila uamuzi wa kuilaumu ikifikiwa.

Utapata kuwa ukoloni mkongwe ulimea mizizi Afrika lakini mizizi hoyo haikung’olewa kabisa kwani ilipitisha ukoloni mamboleo baada ya uhuru wa wafrika. Ingwa nchi za Afrika ziko huru lakini zingali zikitegemea usaidizi wa wakoloni wao wa zamani ambao wamedhibiti nguvu za kiuchumi. Je, ni lini nchi za Afrika zitajinasua na utumwa huu wa kutegemea wazungu? Yote yawezekana kwa umoja wa wafrika ambao ni nguvu thabiti ya kujikombowa kutoka kwa minyororo sugu ya wazungu.