'Naomba Uhuru anipee nyumba'

Sajenti Mstaafu Aron Ojode.

Sajenti Mstaafu Aron Ojode anajulikana kwa majina ya utani kama Jabunde (mtu wa Bunduki) ama Jalweny (Mwanajeshi) na wakazi wa Kijiji cha Majiwa eneo la Kochia kwenye Kaunti ya Homabay. Mzee Ojode, mwenye Umri wa miaka 78, alihudumia taifa kama mwanajeshi kwa miaka 22 huku kilele cha huduma yake ni kwamba alichaguliwa kati ya maafisa 28 waliohojiwa kusimamia ulinzi wa kaburi la Rais wa Kwanza wa Jamuhuri Mzee Jomo Kenyatta mnamo mwaka wa 1978.

Mwanajeshi huyo mstaafu anakumbuka jinsi Mkuu wa Majeshi wakati huo marehemu Jenerali Jackson Mulinge alivyomkabidhi wajibu huo kama afisa wa kwanza kusimamia alipolazwa Mzee Kenyatta na akapewa idhini na bunge kutekeleza wajibu huo kwa muda wa miaka minne.

“Ninakumbuka jinsi nilivyokuwa nikiwakiribisha familia ya Mzee Kenyatta kila mwaka wakati walipokuwa wakija kuweka shahada za maua wakati wa makumbusho, lilikuwa jukumu langu kuwakaribisha viongozi waliokuja kutoa heshima zao kwenye kaburi hilo,” akasema Ojode.

Mwanajeshi huyo mstaafu alisema kuwa wakati alipokuwa akihudumu kwenye wadhifa huo wa kulinda kaburi la mzee Kenyatta alikuwa na makoplo watatu waliokuwa manaibu wake na maafisa 56 wa jeshi waliokuwa wakihudumu chini yake kwa miaka mine aliyohu dumu.

Mzee Ojode alisema kuwa kipindi chake cha kuhudumu kilifikia kikomo ghafla mnamo Agosti 1982 pale jaribio la mapinduzi lililopangwa na Wanahewa lilipofanyika ambapo aliamrishwa na wakubwa wake apige ripoti mara moja kwenye kambi ya kijeshi ya Langata kwa maelekezo.

“Kikosi Changu kiliporipoti kwenye kambi ya kijeshi ya Langata tulipewa jukumu la kuandamana na wenzetu waliokuwa chini ya amri ya Kanali Cheboi hadi Nakuru ili tuweze kumsindikiza Amiri Jeshi wetu Mkuu Daniel Arap Moi hadi Nairobi,” akasema Ojode.

Mwanajeshi huyo mstaafu alisema kuwa Rais Moi alipowasili jijini Nairobi alielekea moja kwa moja hadi kwenye Idhaa ya Taifa ambapo aliwatangazia Wakenya kuwa jaribio la mapinduzi lililofanywa na wanahewa wachache lilikuwa limeangamizwa na nchi ilikuwa na Amani. Mzee Ojode alihudumu kwenye kikosi cha cha Kumlinda Rais kwa miezi 18 ambapo alipata nafasi ya kutembelea sehemu nyingi nchini na hata wakati mmoja aliandamana na Rais Moi katika ziara rasmi nchini Djibouti kabla ya kupata uhamisho hadi chuo cha mafunzo cha kijeshi cha Eldoret alipohudumu hadi alipostaafu mnamo 1/12/1986.

Mwanajeshi huyo mstaafu alisomea shule ya msingi ya Lo-Rateng kati ya 1954 hadi 1957 ambapo aliweza kuyahitimisha masomo yake akiwa darasa la tatu kutokana na changamoto nyingi alizokuwa akipitia nyumbani ambapo aliamia mjini Kericho ambapo alihudumu kama mchunaji majani chai kwa miaka sita. Ojode alirejea nyumbani mwaka 1964 ambapo aliweza kujiunga na Jeshi la Kenya alipohudumu kwa miaka 22 kabla ya kustaafu na kurejea nyumbani ambapo anaishi katika lindi la ufukara licha ya jukumu muhimu alilotekeleza akiwa jeshini kwa muda huo wote. Mzee Ojode ni Mume wa wake wawili( wa kwanza alifariki mwaka jana) na baba wa watoto 12(huku wanne wakiwa marehemu) na pia babu wa wajukuu 27 na anaomba serikali kuweza kumkumbuka na kuisaidia familia yake kwa maana hakuna mtoto wake aliye na kazi ya maana kuweza kukidhi mahitaji ya familia yao.

“Nilipewa malipo ya Sh 75,000 nilipostaafu kutoka jeshini na ninapokea pensheni ya Sh 3,400 kila mwezi ambacho ni kiasi kidogo mno kuweza kukidhi mahitaji ya familia yangu kubwa naomba angalau Rais Uhuru Kenyatta aikumbuke familia yangu ikizangatiwa jukumu nililotekeleza nikiwa jeshini,” akasema Mzee Ojode.

Mwanajeshi huyo mstaafu ambaye kwa sasa anahudumu kama bawabu kwenye makazi ya Mhadhiri Wa Chuo Kiku cha Nairobi marehemu Chrispine Mbai alisema kutokana na mzigo mzito aliokuwa nao wakutunza familia za ndugu zake hakuweza kuwasomesha wanawe vizuri huku wengi wao wakifanya vibarua vidogo vidogo karibu na kwao.

Mzee Ojode alisema kuwa alitumia pesa zake nyingi kuwalea ndugu zake baba yao alipofariki na pia alitwikwa jukumu kuwalea wajukuu wake baada ya watoto wake wanne kuaga dunia na akaomba serikali kuwaajiri baadhi ya wanawe na wajukuu wake Jeshini kama shukrani kwake.

“Kwa sasa mimi ni maskini hohehahe, sina hata baiskeli, ninajua kuwa kuna watu watashanga kuwa Askari Mstaafu kama mimi aliyehudumu Jeshini kwa miaka 22 alipeleka wapi pesa zake zote, lakini ningependa wajue kuwa nilikuwa na mzigo mzito wa kulea sio watoto wangu tu bali pia wa ndugu zangu ambao walikuwa wamefariki tayari,” akasema Mzee Ojode.

Mwanajeshi huyo mstaafu alisema kuwa amehuzunishwa na visa ambavyo nchi ya Kenya imewapoteza wanajeshi wengi nchini Somalia wanapokabiliana na magaidi wa Al Shabaab na akawaomba wawe waangalifu sana wanapotekeleza wajibu wao wa kulinda nchi yetu.