Na Beatrice Maganga
Polisi jijini Nairobi wanawazuilia walimu watano waliokamatwa wakiendeleza mafunzo ya ziada kwa wanafunzi katika Kanisa la House of Grace eneo la Lang'ata. Watano hao wamekamatwa kufuatia taarifa zilizotolewa kwa polisi na wananchi. Katibu katika Wizara ya Elimu Belio Kipsang aliwatuma maafisa wake walioandamana na maafisa wa polisi kutoka Kituo cha Polisi cha Uwanja wa Nyayo kuongoza oparesheni ya kuwakamata.
Ilibainika kwamba wanafunzi zaidi ya hamsini kutoka shule mbalimbali walikuwa katika kanisa hilo wakifunzwa. Ilimlazimu Afisa anayehusika na viwango bora vya elimu John Okiya kuwaagiza wanafunzi hao kuelekea nyumbani.
Wiki iliyopita polisi vilevile waliivamia shule ya HappyLand Praparatory iliyo mtaa wa Buruburu na kuifunga kwa kuendeleza mafunzo wakati wa likizo. Waziri wa Elimu Fred Matiang'i amesisitiza kwamba walimu watakaopatikana wakiendeleza mafunzo hayo watachukuliwa hatua.