Polisi wahusishwa tena na mauaji

Na, Beatrice Maganga

Baada ya kuripotiwa kutoweka takriban wiki moja iliyopita kutoka Kaunti ya Meru, mwili wa muuguzi kwa jina Job Omariba mwenye umri wa miaka ishirini na minane hatimaye umepatikana katika Hifadhi ya Maiti, kwenye Kaunti ya Machakos. Kwa mujibu wa afisa anayesimamia Kitengo cha Kukabili Uhalifu, Noah Katumo, mwili huo ulikuwa na majeraha mikononi na miguuni.
Omariba alitoweka Agosti 21 katika hali ya kutatanisha kabla ya mwili kupatikana eneo la Salama na kusafirishwa hadi hifadhi ya maiti.
Inadaiwa kwamba mwanamume huyo alihadaiwa na mwanamke mmoja kusafiri naye hadi Nairobi ambapo angemsaidia kuimarisha biashara yake. Tayari polisi watatu na dereva mmoja wa texi wametiwa mbaroni kwa kuhusishwa na mauaji hayo.
Kisa hiki kinajiri huku polisi wakihusishwa na kisa tofauti cha mauaji ya mwanamume aliyekuwa amelazwa katika hospitali moja Kaunti ya Kitui.