Na, Sophia Chinyezi,
Shirika la Msalaba Mwekundu limetia saini mkataba wa makubaliano na Shirika la Kitaifa la Sekta za Binafsi KEPSA, ili kukabili ukame unaoshuhudiwa nchini. Akiongoza hafla hiyo mapema leo katika hoteli moja jijini Nairobi, Waziri wa Masuala ya Humu Nchini, Joseph Nkaissery amepongeza hatua hiyo, akisema kuna haja ya serikali ya Kitaifa na zile za kaunti kutenga fedha za kukabili majanga mbalimbali.
Nkaissery ametaja baadhi ya mikakati iliyowekwa na serikali kuwaepushia Wakenya athari za ukame, huku akizipa changamoto serikali za kaunti kuiga mfano wa juhudi hizo na kuanzisha hazina ya kukabili majanga. Aidha amesikitishwa na hatua ya kaunti kujitokeza wakati wa dharura badala ya kujiandaa mapema kukabili majanga endapo.
Kuhusu suala kwamba kila kaunti itatoa shilingi milioni moja kwa Shirika la Msalaba Mwekundu ili kukabili baa la njaa, Nkaissery amesema kiwango hicho ni cha chini mno, ikizingatiwa kuwa ukame umewaathiri zaidi ya watu milioni 1.3.
Kwa upande wake Katibu Mkuu wa shirika hilo, Abbas Gullet amesema kuna mpango wa kuchangisha shilingi bilioni moja ili kushughulikia janga hilo na kuongeza kuwa mikakati ya kusambaza fedha kwa waathiriwa hao imewekwa.