Shoka la DPP Haji kuangukia wengi KPA

Mkurugenzi wa mashtaka ya umma Noordin Haji.

Dukuduku kutokea mianya ya afisi za Mkuu wa idara ya ujasusi nchini George Kinoti na Mkurugenzi wa mashtaka ya umma Noordin Haji zawatia kiwewe miongoni mwa wakaribu wa mameneja wa halmashauri ya bandari nchini (KPA) kwamba lile shoka lililopura Waziri Henry Rotich na mkungo wake wa maafisa wa wizara, huenda likiwaangukia.

Kulingana na habari za ndani, ishara ipo kwamba wengi wao waliopo nyadhifani na wale waliostaafu hivi karibuni kamwe hawana budi ila kutia maji vichwa vyao kwani huenda wakanyolewa kisheria kufuatia mgorogo uliozushwa na tafaruku ya kampuni ya kitaifa ya sheheza za melini, KNSL ambayo yadaiwa kupigwa vita vya ndani kwa ndani kuanzia hapo.

Hofu kuu Habari za kutia hofu zaidi ni mashtaka ya Maneja mmoja Mkuu ambayo yametayarishwa yakiwa jikoni na wakati wowote yataandaliwa mahakamani na maafisa wa upelelezi wa kutoka kwa afisi ya DCI kuhusiana na dai kwamba alishiriki kupora halamashuri zaidi ya shilingi 21 milioni kwa kulipisha sivyo katika huduma za kuokoa meli kinyume na maadili ya bandari na ushuru wa taifa.

Taarifa zaonyesha kuwa uhalifu huu ulifanyika mwezi Desemba mwaka jana wakati meli moja kwa jina la MV Serval International Maritime Organisation iliporipotiwa kuwa na matatizo ya kiufundi na hivyo nahodha wake kuitisha usaidizi wa dharura wa kuvutwa.

Maneja huyu anadaiwa kuandikia barua wamiliki wa meli hii ya MV Serval mnamo tarehe 11 mwezi Januari mwaka huu kudai KPA pamoja na kampuni ya Alpha Logistics zimeafikia kutoza ada ya shilingi 30 milioni kwa huduma za kuvuta ilhali wenye mashua husika zilizotumiwa kuvuta za M Eugene na Nyangumi Two zilikuwa zimeitisha shilingi 51 milioni.

Uchunguzi wa maafisa wa upelelezi ambao ulikamilika mwezi Aprili mwaka huu, umebainisha wazi kuwa meneja huyu analo shtaka la kujibu kwa kutapeli KPA zaidi ya shilingi 25 milioni ambazo zingelipwa halmashauri hiyo na meli husika.

Hadi kufikia hapo, yadaiwa hakuna usingizi kwa maneja huyu kwani hata akisikia paka amekwaruza mlango wake, anashtuka akimdhania ni Noordin Haji na George Kinoti. “Kuna uwezekano wa mameneja wakuu wa bandari ya KPA kuchunguzwa kufuatia mgogoro wa CT2 na kampuni za shehena za meli 5 ambazo zinahudumu bandarini bila mikataba rasmi na halmashauri hiyo.”

Ukiachana na upwaguzi wa kuvuta meli kwa mpigo, kunalo jinamizi lingine ambalo linaendelea kuwakondesha mameneja wengine wakuu wa KPA kuhusiana na sakata la kashfa ya ufisadi wa zabuni ya kampuni ya ujenzi wa kitivo cha mafuta ya Uchina ya China Communication Construction Company.

Hapa mameneja hawa wa KPA wanadaiwa kutayarisha njia ya kujipatia mlungula wa kitita kizito cha njuluku (pesa) shilingi 25 bilioni zaidi ya kiwango halisi cha kazi ambacho kilikadiriwa kwenye kandarasi hiyo kama shilingi 15 bilioni.

Hivyobasi, kulingana na tume ya ufisadi nchini EACC, DCI na DPP, ni wazi uchunguzi umedhihirisha wazi kwamba waliohusika kwenye sakata ya utapeli huu wa pesa za umma hususan maafisa wakuu wa KPA, wanayo kesi ya kujibu kwa kutaka kuhujumu pesa za umma.

Taarifa zaonyesha kuwa kandarasi inayogharimu shilingi 15 bilioni, iliongezwa kihujuma hadi kuwekwa shilingi 25 bilioni na kwa kuwa walikuwa wameanza kupata penyenye ya kupora halmashauri, wakaongeza tena kandarasi hiyo hiyo hadi kutimia shilingi 40 bilioni ndioposa macho ya selikani ikaanza kuikodolea kwa uchunguzi mkali. Sakati hino nayo, inaandaliwa mashtaka yake na wakati wowote, mwewe wa EACC, DCI na DPP huenda akatua makao makuu ya halmashauri ya bandari nchini kuchota wote walioshiriki katika kizungumkuti hiki.

Vita vya KNSL Mburutano baina ya iwapo kampuni ya sheheza za meli ya kitaifa ya Kenya National Shipping Line (KNSL) ni sawa kushirikiana na kampuni nyingine ya kigeni ya MSC kuendesha huduma katika kiegezo cha Container Terminal 2 (CT2) ni halali au siyo halali kisheria, kumezua tumbo joto mpaka kusababisha kuchunguzwa kwa kampuni nyingine bandarini.

Kwa mara nyingine tena, kamati ya bunge, DCI, DPP na tume ya kupambana na ufisadi nchini, EACC wanarudi tena kuchunguza mienendo ya mameneja wa halmashauri ya bandari nchini (KPA), walioko n ahata wale ambao walistaafu ili kieleweke ni vipi kelele zimezidi sasa wakati wa KNSL na MSC kutaka kuanza huduma zake katika kiegesho cha CT2, ilhali kunazo kampuni 5 ambazo zipo bila idhini rasmi ya serikali na zaendelea kutoa huduma za meli bandarini.

Uchunguzi yaaminika unaendelea kuhusiana na kampuni hizi tano ambazo zimekuwepo bandarini zikifanya kazi kwa miaka kadha sasa na uhusiano wake na baadhi ya mameneja walioko na walioondoka ni upi. Katibu mkuu wa chama cha makuli (Dock Workers Union), Simon Sang, hali kadhalika ameorodheshwa kwenye upelelezi huo baada ya kuonekana kupayuka zaidi ya wenye kampuni husika.

Shinikizo la Serikali Serikali nayo inaendelea kushinikiza kamati ya bunge kuwaita wenye kampuni hizi tano hususani ile kampuni nyingine ya kigeni ya Maersk Line inayochukuliwa kuwa pinzani kibiashara na kampuni inayoshirikishwa ya MSC.

Kati yam waka 2007 hadi 2016, kampuni ya Maersk ilikuwa na idhini ya kutumia viegezo nambari 13 na 14 ambapo walitumia fursa hii kujitangaza kibiashara ya shehena ulimwenguni kama wenye fursa ya kuwa na mahala maalum katika bandari ya Mombasa na Afrika Mashariki kwa jumla.

Kulingana na habari za ndani, kampuni hii ya Maersk Line imekuwa ikiitumia sehemu hii ya CT2 kuanzia mwezi April mwaka 2016 baada ya tahatifu (makubaliano) kwamba KPA haiwezi kuitumia, yaaminika Maersk ilingizwa kichinichini kwenye kiegezo hiki bila malipo yoyote na imekuwa ikiendesha shughuli ambazo zinapingwa KNSL na MSC kuendelea nazo.

Licha ya kipengee cha sheria ya nambari 16 kinachopinga huduma za wenye meli na wahudumu kuruhusiwa, ni kampuni hii ya Maersk Line peke yake ambayo inaendesha shughuli zake kupitia kwa kampuni yake nyingine ya Damco kwenye kiegesho hiki cha CT2.

Real Estate
Sustaining single-digit mortgage amid tough economic conditions
Business
Directors wrangles to cost tea farmers Sh560m in lawyers bills
Business
Premium Civil servants face the axe as Ruto seeks to ease ballooning wage bill
Real Estate
Premium End of an era: Hilton finally up for sale, taking with it nostalgic city memories