Mwanaume auliwa Kwale kwa kushukiwa kuugua Korona

Mwanamume mmoja kwenye Kijiji cha Kubundani katika Kaunti ya Kwale ameuliwa baada ya kutuhumiwa kwamba ameathirika na Virusi vya Korona, kisa ambacho kimetokea usiku wa kuamkia leo.

Kulingana na taarifa iliyonakiliwa kwenye Kituo cha Polisi cha Diani, George Kotini Hezron ambaye alikuwa mlevi aliuliwa kilomita tatu kutoka eneo moja la burudani.

Ripoti hiyo imebainisha kwamba kotini alikutana na kundi la vijana lililoanza kumtuhumu kwamba anaugua ugonjwa wa Covid-19 baada ya ugomvi kuzuka baina yake na kundi hilo.

Baadaye, vijana hao walimshambulia kwa mawe na kumjeruhi vibaya na kufariki muda mfupi baadaye alipofikishwa katika Hospitali ya Msambweni. Kamanda wa Polisi wa Kwale Joseph Nthenge amesema msako dhidi ya waliotekeleza unyama huo unaendelezwa.