Tofauti ya 8-4-4 na mtaala mpya wa 2-6-6-3

Wanafunzi wa gredi 3 kutoka shule ya msingi ya Mercy Junior Academy, eneo bunge la Ugenya, kaunti ya Siaya wafanya mtihani wa kitaifa darasani. [Picha: Pambazuko]

Kulingana na ratiba ya mtaala mpya wa elimu nchini Kenya, huu mfumo wa 2-6-6-3, ilikuwa kuanzia tarehe 17 hadi tarehe 20 mwezi huu wa Septemba, wanafunzi wa gredi 3 wanafanya mtihani wa Kitaifa chini ya mtaala mpya wa 2-6-6-3. Baadhi ya shule zimekamilisha mitihani hiyo ambayo ni ya Hisabati na Kiingereza pekee na yenye nembo ya mitihani ya kitaifa kwenye ukurasa wa kwanza.

Kwenye kurasa ya kwanza hiyo hiyo, mwanafunzi alitakiwa kuandika jina lake, nambari yake ya maalum ya mtihani na kuna kuandika jinsia yake kama ni mume au mke, hakuna nafasi ya huntha kwa huu mtaala mpya. Katika huo huo ukurasa wanaendelea kuandika jina la kaunti yao na nambari yake (county code) pamoja na jina la kaunti ndogo wanayotoka na nambari yake pia (sub county code).

Wanafunzi mwisho wanajaza jina la shule na nambari ya shule yao (school code) kisha nafasi ya chini ya mwisho ni ya mwalimu kujaza matokeo kutoka pande zote za mtihani. Kulingana na baadhi ya wanafunzi ambao niliweza kuwahoji, wanasema mtihani huu uliandika.

Hii ina maana kwamba katika huu mtaala mpya wazazi watahusika kwa njia moja au nyengine katika kusaidia watoto kufunzwa shuleni na walimu,hasa kusaidia kukuza talanta za wanao. Mwaka huu ndio mtaala mpya wa 2-6-6-3 ulianza kutekelezwa na haya bado tu ni majaribio ya iwapo mtaala huu utaweza kufanikiwa na kuendelea mbele au la. Kuna mambo mengi zaidi ambayo serikali inahitajika kufanya kwa shule, kwa walimu, wanafunzi na pia wazazi ili kuleta mafanikio mema.

Serikali ina kibarua kigumu kwani inafaa kutafuta mbinu ili kuhamasisha wazazi kuhusu mtaala huu mpya wa 2-6-6-3, wengi hawajaelewa huu mfumo mpya, wanadhani bado ni 8-4-4, pia majukumu yao kamili katika kufanikisha mtaala huu kwa watoto wao hawaelewi. Kwa upande wa walimu kutoka shule za serikali, uandalizi wa karatasi za mtihani huu wa kitaifa wa gredi 3 ni ghali mno.

 ‘’Kuchapisha mtihani hii kutoka kwa mtandao iligharimu pesa nyingi zaidi na serikali haikutoa pesa za mtihani’’, anasema mwalimu mmoja wa gredi 3, Bi Alice Apondo, kutoka shule ya msingi ya Ulawe, eneobunge la Ugunja, kaunti ya Siaya. Walimu wa shule za kibinafsi pia hawakuachwa nyuma katika kutoa kilio chao,wanaomba serikali iwape ufadhili, kuwasaidia kufanikisha mtaala mpya. Wakiongozwa na Bi, Hellen Olesi, maneja wa shule ya msingi ya Mercy Junior Academy, iliyoko mjini ukwala, eneobunge la Ugenya, kaunti ya Siaya wanasema hivi: ‘’Serikali inafaa kutupa usaidizi hasa wa vifaa kama vile vitabu ili kutuwezesha kufunza kwa urahisi huu mtaala mpya, wasituache kivyetu’’.

Mwalimu wa gredi 3 katika shule hii ya kibinafsi ya Mercy Junior Academy, Bi Mildren Akoth, pia alisisitiza kwamba vitabu vinahitajika zaidi darasani ili kufanikisha mafunzo kwa watoto kwani bila vitabu yawa ni ngumu. Kwa ujumla, katika huu mtaala mpya serikali isilale, kunahitajika walimu waliohitimu na kuelewa mtaala huu mpya, wawe wengi na wa kutosha katika kila darasa sababu panahitajika uangalizi wa mwalimu kwa kila mwanafunzi kivyake. Pia yatakiwa mwalimu atakaye anza kufunza wanafunzi katika gredi 1 aendelee nao hadi gredi 3 bila kubadilisha badilisha walimu.

 Hii itawezesha wanafunzi kumwelewa mwalimu wao vyema kando na kumzowea anapowafunza darasani. Baadhi ya walimu wanasifu mtaala huu wa 2-6-6-3 wakisema unafunza walimu kusoma na kuelewa kando na kuwapa wanafunzi nafasi ya kufanya mambo kivyao.

Pia hakuna kabisa kurudia madarasa katika gredi 1, gredi 2 na gredi 3, wanafunzi watakuwa wanaenda wote kwa darasa la mbele, tofauti na mtaala wa zamani wa 8-4-4 ambapo mwanafunzi alikuwa anaweza kurudia darasa limoja hata mara tatu. Wakati wa mtaala wa 8-4-4, wanafunzi ambao walikuwa hawafanyi vyema kwa mtihani waliambiwa warudie madarasa, wengine walirudia mara nyingi hadi wakahepa na kuacha shule kabisa.

 Wanafunzi wanafaa kuhamasishwa vyema kuhusu umuhimu wa huu mtaala mpya na lengo lake, wanafaa kufunzwa kwamba mtaala huu mpya ni mfumo wa 2-6-6-3.

Wanafunzi walianza kwa kufanya mtihani wa hisabati ambao kwa maoni ya wengine ulikuwa mgumu kiasi, palikuwa na maneno mengi ya kusoma ndipo uweza kuelewa na kufanya hesabu. Kwa mtihani wa somo la kiingereza hapakuwa na ugumu wowote, wanafunzi walisoma hadithi fupi na kujibu maswali, kujaza mapengo, kusoma maneno na pia kuandika tungo, “Composotion’’. 

Kuna mabadiliko makubwa sana katika somo la hisabati kwa sababu hesabu ambazo zilifunzwa kwa shule ya upili ndio zimeundwa na kuletwa kwa wanafunzi wa gredi 1, gredi 2 na gredi 3. Pia kuna hesabu zingine za kigeni ambazo hata wazazi waliosoma hadi kidato cha nne sasa hawawezi kufanya bila kuelekezwa.Wazazi wanashauriwa wasiwafunze wanao hesabu nyumbani kwasababu watawachanganya kwa kutumia mbinu zingine ambazo hazifai au za kizamani. Jukumu la wazazi kwa wanafunzi litakuwa ni kuwapa mahitaji mengine ambayo yanatakikana shuleni kusaidia mwalimu kufunza.