Nitastaafu siasani iwapo nitashindwa 2022 -Ruto

Naibu wa Rais William Ruto amesema yu tayari kustaafu siasani iwapo atashindwa kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka wa 2022.

Aidha, Ruto amesema uongozi wa Chama cha Jubilee utajadili kuhusu atakayepeperusha bendera ya chama hicho katika kinyang'inyiro cha urais vilevile nyadhifa nyingine za kisiasa. Vilevile, amesisitiza kwamba iwapo hatateuliwa kupeperusha bendera ya chama hicho, atamuunga mkono yeyote atakayeteuliwa kwani si lazima awe debeni mwaka wa 2022.

Akihojiwa na redio moja nchini, Ruto aidha amesisitiza kauli yake kwamba hakuna Mkenya wala kiongozi yeyote ambaye ana deni la mwingine la kisiasa hasa siasa za mwaka wa 2022.

Ruto ameweka wazi kwamba hatakubali Wakenya kupigana kwa sababu ya siasa za chuki na kabila.
Wakati uo huo, Ruto amewasuta viongozi ambao wanajifanya kuyajali maslahi ya Wakenya ilhali ni watapeli wa kisiasa ambao wanalenga kujinufaisha.

Amesema yeyote atakayeshindwa kwenye chaguzi zijazo sharti akubali huku akiwasuta wabunge wa kundi la Kieleweke kwa kueneza propaganda kwamba wafanyabiashara kwenye eneo la Kati watapokonywa mali yao iwapo atatwaa urais.

Related Topics

Ruto 2022 Siasa