Kivutha Kibwana atishia kuishtaki Kampuni ya Kenya Pipeline

Gavana wa Makueni, Kivutha Kibwana anatishia kuishtaki Kampuni ya Mafuta ya Kenya Pipeline katika Mahakama ya Kimataifa kwa kukosa kusuluhisha visa vya umwagikaji wa mafuta kwenye maeneo tofauti tofauti ya kaunti hiyo, iwapo kisa cha hivi punde cha kiboko hakitasuluhishwa upesi.

Akizungumza katika mkutano na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa KPC, Hudson Andambi na wakazi kwenye eneo la Kiboko ambako mafuta yamemwagika, Kibwana anasema imechukua muda mrefu kusuluhisha kisa cha Thange na kufikia sasa miaka mitatu baadaye, suluhu mwafaka haijapatikana, na sasa anataka fidia kwa wakazi wa Kiboko ambao sasa wanaathirika.

Kibwana anataka wakazi hao wapate maji kwa muda ambao maafisa wa KPC wataendeleza shughuli za kuchunguza maji na mchanga wa eneo hilo, akisema wakazi hao wanategemea maji kunyunyizia mboga na matunda ambayo yanauzwa nje ya nchi, na pia wapate maji ya kutumia nyumbani, pamoja na kupimwa katika zahanati ili ibainike iwapo watu hao tayari wameathirika na mafuta hayo.

Kwa upande wake, Mkuu huyo wa KPC amewaomba radhi wakazi hao kwa umwagikaji huo na kuwaahidi kuwa maafisa wake wanaendeleza uchunguzi huku akiomba muda wa kutathmini hali  kisha uamuzi utafanywa kuhusu masuala yote ya fidia na usaidizi.