Wanawiri kwa vipepeo na unga kutoka kwa mchicha

Amos Mwamburi achuchumaa kuingia katika mimea pori minene iliyojiviringa ndani ya ngome iliyotengenezwa na wavu. Anafikia jani moja pana na kuligeuza, kwa ukaribu sana analifanyia utafiti wa uso wake. Anapiga hatua kwa mmea unaofuata na kurudia uchunguzi huo huo. Mwisho wa nyuma ya ngome, vijana wawili wa kiume wameinamia mimea ya maua, wakiyaangalia majani kwa makini na ustadi.”

“Nimepata kadhaa hapa,” Bwana Mwamburi atoa wito. Upande wa chini wa jani aliloshika, anaonyesha vijitu vingi duara na rangi ya kijivu-nyeusi, mayai ya vipepeo, vimeingia na kujishikilia imara juu ya uso wa kijani. Anakwanyua jani kwa umakini kutoka kwa shina na kuliweka ndani ya ndoo ya plastiki.

Picha: Amos Mwamburi

Mwamburi ni mmojawao wa wanachama 14 wa kikundi cha vijana Chawia ambao wamechukuwa tahadhari ya wengi baada ya kuanzisha kilimo cha vipepeo maeneo ya milima Chawia kaunti ndogo ya Mwatate. Kikundi hicho kilianzisha mradi huu kabambe kama njia ya ubunifu kupata kipato ili kujiendeleza kimaisha huku wakikuza hifadhi ya mazingira.

Sehemu ya hifadhi hio inafikiwa kwa kupanda majani ambayo yanaongeza uoto na kuruhusu urejesho wa kufunguliwa kwa idadi ya vipepeo katika milima ya Taita. Wanachama hao waliojifunza wenyewe wanasema kilimo cha vipepeo ni sanaa ya maridadi inayohitaji ujuzi maalum. Mwamburi anaelezea kikundi kilivyoamua kutumia soko la watoto vipepeo lililo na faida kubwa kama njia ya kujipatia kipato na kuendeleza hifadhi dhidi ya kukata miti kiholela ambayo kwa sasa imeweka hatarini vipepeo vya aina fulani.

Ingawaje eneo hilo lina aina tofauti za vipepeo, kikundi hicho kina nia ya kutengeneza soko zuri kwa kulenga aina mbili za vipepeo kwa majina Papilio Desmondi almaarufu kama ‘Green-branded swallowtail’ na Geometrid moths ambao wanapatikana eneo hilo pekee.

“Tunataka kutengeneza jina kupitia aina ya vipepeo wanaopatikana Taita pekee ili kuzuia hasara wakati vipepeo watajaa kwa wingi kwenye soko,” alisema.

Uamuzi wa kulenga ufugaji wa aina hizo za vipepeo umepelekewa na hasara kubwa ambayo kikundi kilipata mwezi Decemba mwaka 2018 baada ya soko kufa. Wanunuzi kutoka Gede Malindi walisema soko limeenda chini.

“Ilikuwa hasara kubwa sana kwetu kwani tulikuwa na watoto vipepeo zaidi ya 2000 tayari kupeleka sokoni. Kwa bahati mbaya, wakulima ya Gede walikuwa na aina hio hio tuliyokuwa nayo kwa hivyo ikatubidi kuachilia wetu warudi msituni kwani tayari walikua vipepeo,” alisema.

Kikundi kilitarajia kutengeneza shilingi 50,000 na kikapata shilingi 12,000 tu baada ya kuuza rejareja kila mtoto kipepeo mmoja kwa shilingi thelathini.

Vikundi kadhaa vya hifadhi wamewapongeza wafugaji vipepeo na kuawataka waendelee na mori huo huo. Nature Kenya, shirika lisilo la serikali linalolenga kuokoa ndege nadra wanaopatikana Taita, walitolea kikundi hicho wavu na mirija ya kukamatia vipepeo porini. Pia, kikundi kilipata mafunzo kutoka kwa mtaalum wa vipepeo wa mradi wa kipepeo Arabuko Sokoke.

Wanachama wanawinda vipepeo wa kike ndani ya msitu Chawia. Mwamburi anaelezea kuwa vipepeo wa kike wanawajua kwa urahisi kwa sababu ya tabia yao kuruka jani hadi jani wakitafuta mahali pa kutaga mayai.

Wakitumia maji ya sukari au maji ya massa ya ndizi kama chambo kwa vipepeo, wanachama wanashika wengi ajabu. Vipepeo wanafungiwa ndani ya ngome ya wavu ambapo mimea tofauti imepandwa. Baada ya kutaga mayai, vipepeo huachiliwa kurudi porini. Kikundi hupata mayai mengi kama 200 kutoka kwa kipepeo mmoja.

Mwamburi alisema aina tofauti za vipepeo wana upendeleo tofauti wa mimea fulani.

“Baada ya kuangua mayai, ndani ya wiki moja, mabuu hula kwa majani hayo. Mtu anastahili kuwa na mimea sahihi sivyo mabuu yatafuka,” alieleza.

Ili kushinda changamoto ya kulisha mabuu, kila mwanachama anatakiwa kukuza aina fulani ya mimea ya majani ya vipepeo nyumbani kwao ili kuweka chakula tayari wakati mayai yanaangua. Mimea inayopendelewa ni ya machungwa na malimau.

Wakati mabuu hula chakula kingi ndani ya wiki tatu na nne kabla kuwa watoto vipepeo waliokomaa tayari kupelekwa sokoni.

Alisema kupata soko bado ni changamoto kubwa kwa kikundi. Wanawauzia watu rejareja ama maafisa wa ufugaji vipepeo wa Gede. Mtoto kipepeo mmoja huuzwa kwa shilingi hamsini lakini wanapowauzia watu rejareja huwa shilingi thelathini.

“Hatuna namna kwa sababu hatuwezi fikia soko letu,”alisema.

Wanapokuwa tayari, kikundi hicho hupakia watoto vipepeo kwenye vifurushi maalum na kuwasafirisha kutumia G4S au Wells Fargo kwa wanunuzi wa Malindi ambao baadae huuza nje ya nchi. Wakati mwengine, wanapata hasara endapo mtoto kipepeo atakomaa na kuharibu wengine wote.

Maafa kama hayo hutokea kutokana na ukosefu wa kujua kinachosababisha kila mara mayai huangua. Mayai hukotwa muda tofauti na kuangua muda tofauti. Jambo hili hupelekea ukosefu wa soko kwa sababu kundi dogo la mayai huangua wakati tofauti.

Mwamburi alieleza buu linapokomaa na kuwa mtoto kipepeo, anastahili kusafirishwa kwenye soko haraka upesi. Alinadi kwamba ni ghali kusafirisha watoto vipepeo kidogo kila mara.

“Tunajaribu tupate vipepeo wote watage mayai kwa wakati mmoja ili tupate watoto vipepeo kwa wakati mmoja,” alisema.

Gilbert Obunga, mtaalam wa Nature Kenya, alisema shughuli kama hizo huchangia hifadhi huku zikiwawezesha wanajamii kiuchumi. Alinadi endapo na kama soko lingekuwa zuri, kikundi kingeweza pata zaidi ya shilingi 20,000 kila wiki kwa kuuza watoto vipepeo.

Kipepeo

Aliongezea kwamba wakulima wakiendeleza shughuli kama hizo, misitu na mimea yote ya misituni itahifadhiwa vizuri huku mingine zaidi ikipandwa kwa ajili ya vipepeo.

“Hii ndio kesho ya hifadhi ambapo kila mwanakijiji atapata kipato bila ya kuharibu mazingira,” alisema.

Bwana Obunga, ambaye shirika lake linapigana vita dhidi ya kuokoa aina mbili muhimu ya ndege; Taita Apalis na Taita Thrush, alisema kilimo cha vipepeo kinahamasisha utunzaji wa mazingira yanayoruhusu aina zengine kustawi.

Unga wa mchicha waenua mapato ya kikundi Kisauni

Hakuna asiyejua mmea wa mchicha na hasa matumizi ya majani yake kama mboga kabambe inayopendwa na kupendekezwa kama chanzo imara cha virutubisho.

Lakini pengine ni wachache wajuao kwamba mbegu zake, ambazo hujitokeza na kuundika kama mfano wa shungi kwenye mmea huo, laini na rangi ya kijani iliyochujika, pia inaweza kutumika kama chakula.

Na pengine kutokujua huku huwafanya wengi kuzitupa mbegu hizo kwa dhana ya kwamba hazina faida yeyote. La hasha.

Kikundi kimoja kinachotambulika kama Wakesho CBO eneo la Kisauni kaunti ya Mombasa, walijifunza kutumia mbegu za mchicha kama kitega uchumi kwa kutengeneza unga wenye matumizi mbalimbali ya kiupishi. Unga huu wa mchicha - Amaranth flour kimombo - unaweza kupikia uji, kuongezwa kama kiungo kwenye supu na pia huchanganywa kwa unga wa ngano kwa mapishi ya chapati, mahamri na vinginevyo.

 Wakesho ni kikundi kinacho jishughulisha na kazi za kuinua jamii hususan kuwasaidia mabinti au wasichana ambao wanatoka kwenye familia masikini kwa kuwapatia mafunzo mbalimbali. Ni kazi hii yao ndio iliwapeleka katika biashara hii ya unga wa mchicha kwani ni njia mojawapo ya kutengeza hela ambazo zinafadhili miradi yao.

Kulingana na kiongozi wa kikundi hicho Jane Mbinga, walipata usaidizi kutoka kwa wizara ya ukulima kuambatana na matumizi ya unga wa mchicha mnamo mwaka wa 2014.

“Huwa tunakusanya mbegu hizo za mchicha kutoka kwa wakulima , halafu tunaziosha na kuzikausha juani hadi zikauke kabisa na kutoka unyevu wote. Baadaye tunazipeleka kwa mtambo wa kusaga na tunapata unga,” alieleza mama huyo.

Halafu wanapakia unga huo kwenye mifuko ya nusu kilo na kuuzwa shilingi 150 kwa pakiti moja. Kwa mujibu wa jamaa hawa, mbegu hizo za mchicha zikikaushwa vizuri kabisa vile ipaswavyo kabla ya kusagwa unga wake unaweza kukaa hadi miezi miwili bila kuharibika.

“Unga wa mchicha umejaa kirutubisho cha calcium, na pia unaongeza uwezo wa kinga mwilini dhidi ya maradhi pamoja na kwamba una safisha damu. Ni chakula bora sana,” alisema Mbinga.

Na pengine chakushangaza ni kwamba, kikundi hicho kinadokeza kwamba hizo mbegu za mchicha huwa pia wanazipika zikawa ‘pop corns’, ambazo hizi huuzwa shilingi 30 kwa pakiti moja. 

Na mbali na kuwa kikundi hicho kinajihusisha na biashara ya bidhaa nyingine, mama Mbinga anaeleza kwamba huu unga wa mchicha umetokea kuwa kitega uchumi chao muhimu kutokana na uuzaji wake mkubwa.

“Sisi pia hutengeza vikoi lakini unga huu umekuwa ukiuza vizuri sana kwa sababu ni chakula na hata mara nyingine mapato ya unga wa mchicha hutusaidia kuongeza mtaji wa utengezaji vikoi,” alidokeza.

Kikundi hiki kinauza takriban kilo 150 za unga huo kila mwezi, isipokuwa gharama za uzalishaji pia ziko juu kwa sababu mbegu za mchicha zinaagizwa kutoka sehemu za mbali kama vile Mpeketoni kaunti ya Lamu, Taveta na hata Siaya magharibi mwa Kenya.

“Usafirishaji unatuumiza sana. Kwa mfano kusafirisha kilo 200 za mbegu hizi kutoka Mpeketoni mpaka Mombasa inagharimu hadi shilingi 1500. Na tena bado tutalipa vibarua kutusafishia hiyo mali, pamoja na gharama za kusafirisha tena hadi mtamboni na kurudi na kupakia,” alieleza.