Kasisi ashtakiwa rasmi kwa makosa ya kumtishia mwanahabari

Mhubiri wa Kanisa la Neno Evangelism, James Ng'ang'a ameshtakiwa kwa kumtishia maisha mwanahabari wa runinga ya Citizen, Linus Kaikai na kuachiliwa kwa dhamana ya shilingi laki mbili.

Ng'ang' amefikishwa katika Mahakama ya Kiambu baada ya kuzuiliwa katika Makao Makuu ya Idara ya Upelelezi - DCI, baada ya kukamatwa Jumapili wiki iliyopiya kwa kumtishia maisha Kaikai pamoja na kuchochea ghasia.

Kiongozi huyo wa kidini alitoa vitisho hivyo kupitia kanda ya video iliyosambazwa pakubwa katika mitandao ya kijamii huku akijiita “Chief General Commander” na kutoa vitisho dhidi ya Kaikai bila ya kufafanua hatua ambazo angechukua.

 

Vitisho hivyo vilitolewa kufuatia kauli ya Kaikai kuwa ni wakati serikali iweze kuwadhibiti wahubiri nchini ambao anasema asilimia kubwa wamekuwa wakiwalaghai wananchi mamilioni ya pesa.