Waziri Amina aanza rasmi majukumu katika Wizara ya Michezo

Waziri mpya wa Michezo, Tamaduni na Turathi Balozi Amina Mohammed asubuhi hii amechukua rasmi wadhifa huo kutoka kwa mtangulizi wake Rashid Echesa. Hafla ya kumkabidhi mamlaka imefanyika katika makao makuu ya wizara hiyo kwenye jumba la Kencom, mjini Nairobi.

Ikumbukwe Echesa alisimamishwa kazi na Rais Uhuru Kenyatta wakati alipofanya mabadiliko katika Baraza la Mawaziri Ijumaa wiki iliyopita. George Magoha alichaguliwa kuchukua nafasi ya waziri Amina kwenye Wizara ya Michezo. 

Wataalamu wa masuala ya siasa wamesema kubanduliwa kwa Echesa kulibainika mwaka jana wakati Rais alimkaripia kufuatia hali mbaya ya kaburi la marehemu Jaramogi Oginga Odinga mjini Bondo.

Baadaye alijipata katika mivutano kadhaa kukiwemo kuhusishwa na jaribio la kumkashifu Seneta Cleophas Malala kwa kuchapisha picha bandia mtandaoni akiwa na mwanamke. Hata hivyo baadhi ya wataalamu wanasema huenda ametumika kuwa mfano kwa mawaziri wengine fisadi.