Rais Kenyatta ajiandaa kuapishwa

Na, Beatrice Maganga
Rais Kenyatta ajiandaa kuapishwa
Rais Mteule Uhuru Kenyatta ajilitokeza kisha kutembea kutoka ofisi yake iliyo katika Jumba la Harambee jijini Nairobi hadi lile la Treasury kwa mkutano. Baadhi ya wananchi walibahatika kumsalimu Rais. Katika mkutano huo, Uhuru alifanya mkutano wa washikadau katika sekta ya uchumi ikiwa ni mojawapo ya mipango yake ya kuandaa ajenda za kushughulikia katika kipindi cha pili cha uongozi wake.
Mkutano baina ya Rais na washikadau hao ni watatu kufanyika kwa kipindi cha wiki tatu zilizopita. Mikutano hiyo ilianza punde Tume ya Uchaguzi, IEBC ilipomtangaza kuwa mshindi wa marudio ya uchaguzi wa urais. Tayari amefanya mikutano na washikadau wa sekta ya kawi na maji.
Anatarajiwa kuzizungumzia ajenda alizo nazo kwa wananchi atakapoapishwa rasmi kuchukua hatamu za uongozi siku ya Jumanne katika Uwanja wa Kasarani, jijini Nairobi. Wanajeshi wanaendelea na mazoezi ya hafla ya kumwapishwa katika uwanja huo huku kamati-andalizi ya shughuli hiyo ikisema inatarajiwa kwamba wageni zaidi ya laki moja watahudhuria.

Related Topics