Viongozi wapya wanaojiunga na Idara ya utumishi wa umma wameagizwa kutangaza wazi mali zao chini ya kupindi cha siku 30 kabla ya kuingia ofisini.
Kupitia taarifa, Tume ya Maadili na Kukabili Ufisadi, EACC imesema hatua hiyo ni hitaji kwa viongozi wote wanaojinga na kazi za umma kulingana na sehemu ya 26 na 27 ya sheria za maadili kuwahusu maafisa wa umma.
Endapo watakosa kufanya hivyo ama kudanganya kuhusu mali zao, basi hilo litakuwa kosa la uhalifu na huenda wakatozwa faini ya shilingi milioni moja ama kifungo cha mwaka mmoja jela.
Tume ya Huduma za Umma, inaeleza kuwa mali za viongozi zinastahili kuwekwa wazi chini ya siku 30 punde tu baada kuanza majukumu ya huduma kwa umma.
Wanaolengwa zaidi ni viongozi ambao wamechaguliwa kwa mara ya kwanza wakati wa uchaguzi wa Agosti.
Miongoni mwa masuala ambayo yanastahili kuwekwa wazi wakati wa shughuli hiyo ni kiwango cha pesa wanazolipwa, pesa walizo nazo katika akaunti za benki, mali mfano mashamba, nyumba na magari kila baada ya miaka miwili. Aidha, wanastahili kuweka wazi mali za wake zao, wapenzi na watoto walio chini ya umri wa miaka 18.