Premium

Mwili wa Tom Okwach mmoja wa wachimba migodi waliofukiwa na mchanga wakiwa hai ndani ya Mgodi wa Abimbo umepatikana miezi saba tu baada ya kisa hicho kuripotiwa katika kaunti ya Siaya.

Hali ya mkanganyiko wa hisia imeshuhudiwa nyumbani kwa Tom Okwach mmoja wa wachimba migodi waliofukiwa na mchanga wakiwa hai ndani ya chimbo la Abimbo, katika Kaunti ya Siaya baada ya mwili wake kupatikana miezi saba tangu alipotoweka.

Familia ya marehemu imesema imefurahi kupata mwili wa mpendwa wao licha ya kujawa na huzuni wakati mabaki ya mwili huo yalipokuwa yakitolewa.

Ndugu wa Okwach, Steve Aliwa, amesema mwili huo umepatikana alfajiri ya Jumapili kufuatia juhudi za  wachimba migodi waliokuwa wakiendelea na shughuli zao wakiwa bado na matumaini kwamba huenda wangeupata mwili wa marehemu.

Okwatch alifukiwa ndani ya mchanga akiwa hai na wenzake 9, tarehe 2 mwezi Desemba mwaka uliopita.

Saba walipatikana wakiwa hai huku mmoja akifariki dunia.

Familia ya Okwach imekua ikiutafuta mwili huo licha ya serikali ya kitaifa na ile ya kaunti kukata tamaa baada ya kuutafuta kwa wiki kadhaa.

Hata hivyo, familia hiyo ilikataa kuzika mgomba wa ndizi kama ishara ya mazishi ya kufiliwa kulingana na mila za Jamii ya Dholuo, na badala yake kuwa na matumaini kwamba mwili wa mwanawe ungepatikana.