Hivi majuzi, tumeshuhudia mabadiliko ya kisiasa katika mataifa mbali mbali ulimwenguni. Kati ya mabadiliko haya ni kung'olewa mamlakani kwa viongozi ambao wamekuwa mamlakani kwa muda mrefu. Vile vile vyama vya kisiasa ambavyo vimekuwa katika upinzani vimeweza kutwaa hatamu za uongozi.
Hapa barani Afrika ni nadra sana kwa rais aliye mamlakani kushindwa katika uchaguzi hadi aamue yeye mwenyewe kutogombea kiti cha urais. Hili ni jambo ambalo linaonekana kuwakera watu wengi na kulingana na hali ilivyo kwa sasa, huenda mtindo huu wa kiimla ukakomeshwa na wapigaji kura.