Nairobi, Mombasa na Mandera kufungwa kwa siku 30

Matarajio ya wengi kwamba Rais Uhuru Kenyatta angelegeza masharti ya Kudhibiti Maambukizi ya Korona kwa lengo la kufufua uchumi wa taifa, yamepata pigo baada ya masharti hayo kuongezwa.

Tukianza na mafuku ya kusafiri kwenye kaunti mbalimbali - Marufuku ya kuingia na kutoka kaunti za Nairobi,  Mombasa na Mandera yameongezwa kwa siku nyingine thelathini huku Kilifi na Kwale zikifunguliwa kuanzia kesho saa kumi alfajiri.

Katika hotuba yake iliyosubiriwa na Wakenya kwa hamu kuu, Rais Kenyatta amesema amri ya kutokuwa nje kuanzia saa moja usiku hadi saa kumi na moja alfajiri itaendelea kutekelezwa japo kuanzia saa tatu usiku hadi saa kumi alfajiri.

Rais amesema hatua ya kubadili muda wa amri ya kutokuwa nje imechukuliwa ili kuwapa nafasi Wakenya kuanza kurejelea kazi zao wakati wa mchana ili kujitafutia riziki.

Hayo yamejiri huku Rais akiondoa marufuku ya kuingia na kutoka kwenye mitaa ya Eisleigh hapa Jijini Nairobi na Old Town jijini Mombasa akisema masharti hayo yalisaidia katika kukabili maambukizi zaidi.

Wakati uo huo, Rais Kenyatta amesema alilenga kuyalegeza masharti yote japo wataalamu wakatoa mapendekezo ya kuhimiza mikakati zaidi kuwekwa kabla ya kulegeza masharti hayo. Amesema makundi mawili yenye mitazamo tofauti yaliibuka miongoni mwa wanachama wa kamati hiyo, hivyo kuafikiana kufanya maslahi ya Wakenya kipaumbele.

Amesema hali ya kuongezeka kwa visa vya mambukizi ya virusi vya Korona katika maeneo mbalimbali nchini siku za hivi karibuni, imebadili mipango ya kutaka kufufua uchumi kwa sasa.

Hayo yamejiri huku watu ishirini na sita wakithibitishwa kuambukizwa Korona katika saa ishirini na nne zilizopota, na kufikisha idadi jumla ya maambukizi nchini kuwa elfu mbili na mia sita.

Hata hivyo, watu wengine wanne wamethibitishwa kuaga dunia kutokana na Korona, na kufikisha idadi ya jumla ya waliofariki kuwa themanini na watatu.

Miongoni mwa masuala matatu makuu yalioangaziwa na kamati ya Kitaifa ya Dharura ya Kushughukikia Janga la Virusi vya Korona, wakati wa kupendekeza kuongezwa kwa masharti hayo, kwanza - ni iwapo visa vya maambukizi ya Korona kila siku vinapungua au la, ambapo ni bayana kwamba vimekuwa vikiongezeka kulingana na wingi wa sampuli zinazopimwa kila siku.

Pili, ni utayarifu wa kaunti mbalimbali katika kuwahudumia walioambukizwa Korona, ambapo Rais amesema kila kaunti inafaa kuwa na angalau vitanda mia tatu ili kufanikisha mpango wa kulegeza masharti hayo.

Vilevile suala la tatu lililozingatiwa, ni iwapo kila Mkenya ana uwezo wa kumlinda aliyeambukizwa Korona akiwa nyumbani, endapo virusi hivyo vitazuka kwa mara nyingine baada ya kufungua uchumi kisha kuwazidi wahudumu wa afya.

Kulingana na ripoti ya kamati ya kushughulikia Korona, ni kwamba asilimia ya maambukizi imeongezeka hadi 3.1 kutoka asimilia 2.1 tangu serikali ilipotangaza marufuku ya awali kuanzia tarehe 16 mwezi Mei.