Joho aokoa sura za wabunge mbele ya Uhuru

Rais Uhuru Kenyatta akiwa na Gavana wa Mombasa Hassan Joho (katikati) na Mwenyekiti wa Uchumi wa baharini Jenerali Samson Mwathethe (kushoto) wakizuru idara ya uhandisi katika uzinduzi wa Bandari Maritime Academy

Baadhi ya wabunge wa pwani ambao walijitokeza kwenye sherehe ya Rais Uhuru Kenyatta ya kuzindua sekta muhimu ya mafunzo ya ubaharia katika kitengo cha uchumi samawati, yadhihirika kuwa walihudhuria shingo upande.

Hii ni baada ya mpango wao wa kumtaka kumrai gavana wa Mombasa, Hassan Joho jioni yake kabla ya uzinduzi wa Bandari Maritime Academy, wa kumtaka asusie ama kuwa muongozo juu ya kuhudhuria au la, kutibuka.

Wabunge chungu nzima wa pwani wakiongozwa na Abdulswamad Nassir wa Mvita ambamo uzinduzi huo ulifanyika, wamekuwa katika mstari wa mbele kuhakikisha kufaulu kwa mradi huu umefilisishwa aidha kimawazo ama kuhusudiwa na viongozi waliochaguliwa.

Yaaminika jioni ya siku ya Jumapili kuamkia Jumatatu ya uzinduzi, wote walikusanyika kukutana na gavana ambaye licha ya kuwapa sikio la kuwasikiza maunyeunye yao, yeye hatimaye aliendelea na ratiba ya Rais kama kiongozi mwenyeji.

“Kweli tulikutana kama wabunge kwa gavana na kuapa kwamba hatuwezi kuhudhuria sherehe hizi lakini yote hayo yamekuwa ni mjango tu, nimeona mimi binafsi nihudhurie kumpa nguvu gavana wangu mbele ya Rais Uhuru Kenyatta,” asimulia mbunge wa Jomvu, Badi Twalib aliponukuliwa akizungumza na waandishi wa habari wa karibu naye.

Na kweli jinsi walivyoingia ukumbini wa uzinduzi siku hiyo, walionekana kana kwamba walikuwa hawajajitayarisha kikamilifu na sherehe hizo. Kutokana na ripoti za awali kwa waandalizi wake, kwanza walikuwa wamejikuta kwenye njia panda iwapo wabunge watafika kutokana na msimamo wao mkali ama wataukwepa mkutano huo wa rais.

Kama haingekuwa jitihada za mwenyekiti wa kamati kuu ya Uchumi samawati (Blue Economy), Jenerali Samson Mwathethe, yamkini kamwe hawangepata hata mwaliko kutokana na hofu ya waandalizi kwamba huenda wakazua madharau.

Mwathethe yasemekana alisisitiza wabunge wote waalikwe ili kuona nani halisi ni maadui wa manufaa ya jimbo. Kwa upande wa gavana na mwenyeji wa Rais, Hassan Joho, alihusishwa mapema juu ya sherehe za uzinduzi kupitia kwa mwenyekiti wa uchumi samawati Samson Mwathethe na Rais Uhuru Kenyatta na yasemekana ilimbidi yeye mwenyewe kukatiza safari yake ya ng’ambo ili kujumuika na rais na kushuhudia uzinduzi huo.

Wadadisi wa masuala ya mwambao wanasema kuwa kuwepo kwa gavana Joho kulisaidia pakubwa kupunguza lawama na aibu kwa wabunge waliohudhuria sherehe za uzinduzi wa chuo cha Bandari Maritime Academy.

Miongoni mwa wabunge waliokuwepo walionekana wanyonge kwa fedheha za kupinga mswada unaohusiana na huduma za shirika la shehena za bandarini nchini la Kenya National Shipping Line (KNSL) bungeni.

Waliopata fursa ya kukaa jukwaani la rais pamoja na magavana watatu wanaokurubana na ufuo wa bahari hindi moja kwa moja, Hassan Joho (Mombasa), Salim Mvurya (Kwale) na Fahim Twaha (Lamu), walionekana kana kwamba wamekalia viti vyenye misumari ama miba wakibabaika kwamba huenda msemaji mmoja hadi mwingine anayetoa hutuba anaweza kuwakejeli.

Wanyenyekea wote

Wale waliokuwa werevu kama mbunge wa Likoni, Mishi Mboko, Teddy Mwambire (Ganze), Omari Mwinyi (Changamwe), Badi Twalib (Jomvu), Jonas Mlolwa (Voi) Ken Chonga (Kilifi Kusini), William Kamoti (Rabai), Naom Shaban (Taveta) na Danson Mwashako (Wundanyi) walijibidisha hata hivyo kuhakikisha wameonekana vilivyo kutoa hofu kwamba wamejiunga rasmi na jitihada za kuona kwamba manufaa ya uchumi huu umefikia kila pembe ya pwani na taifa zima kwa ujumla.

Wawakilishi wa kina mama waliokuwepo ni Mama Asha (Mombasa), Getrude Mbeyu (Kilifi), Lydia Haika (Taita Taveta) na Ruweida Obbo (Lamu). Maseneta walioambatana na magavana hawa watatu ni pamoja na mbishani mwingine mkuu wa mradi huo Mohamed Faki (Mombasa), Issa Boy (Kwale) na seneta wa Lamu Anwar Loitiptip.

Akikwepa siasa ya mgawanyiko, katika hutuba yake ya kumkaribisha rais, gavana wa Mombasa badala yake alitoa ujumbe kwa viongozi wote wa upinzani na serikalini kwamba wakati wa mbwembwe za kisiasa umepita na ndio maana yeye anamuenzi rais Uhuru Kenyatta na kwamba iwapo kunalo jambo la kukera ni vyema viongozi wazungumzane kuliko kupayuka.

Uzinduzi wa Bandari Maritime Academy na ufuzi wa sekta ya uchumi wa baharini anasema umetoa changamoto mpya kwa viongozi wa pwani hususani waliochaguliwa hususan magavana wote sita wa Mombasa, Kwale, Kilifi, Tana River, Lamu na Taita Taveta.

Joho alimurai na kumtaka mwenyekiti wa kamati kuu ya uchumi wa baharini Jeneral Mwathethe kutumia bakora aliyotumia kushinikiza ufanisi huu kwa kuwaleta pamoja magavana wote wa jimbo ili kuona kwamba wamejumuika katika kutekeleza na kufanikisha wazo hili muhimu kwa uchumi wa kaunti zote hizi.

“Uzinduzi wa chuo hiki ni mwamko mpya kwetu sote kama jimbo lenye kukurubana na bahari hindi. Takuomba mwenyekiti na ndugu yetu mkubwa Jeneral Mwathethe, usichoke nasi, jaribu kutuleta sisi magavana sita pamoja chini ya mwenyekiti wetu hapa wa Jumuiya ya Kaunti za Pwani, gavana wa Kwale, Salim Mvurya ili tuchangamkie kwa pamoja,” Joho alitoa hakikisho kwa Rais Uhuru Kenyatta.

Wakati huo huo, anasema magavana wanafaa kuonyesha mfano mzuri kwa kuweka vichwa pamoja na kuona kuwa mafunzo ya ubaharia yamewafikia vijana chungu nzima wanaohitaji taaluma mbali mbali za kuwafanikisha kufanya kazi melini.

“Sisi kama magava hatushindwi kila kaunti kuchanga kiwango cha shilingi milioni tano kuhakikisha zimeingia kwa mfuko wa mafunzo wa vijana watakaosomea hapa Bandari Maritime Academy,” asisitiza Joho.