Margaret Kobia amtetea Passaris dhidi ya makabiliano na Gavana Mike Sonko

Waziri wa Huduma za Umma na Masula ya Vijana na Jinsia, Margret Kobia amemtetea Mwakilishi wa Kike wa Kaunti ya Nairobi, Esther Passaris dhidi ya makabiliano ya maneno baina yake na Gavana Mike Sonko wakati wa hafla ya Madaraka.

Utetezi huu unajiri baada ya Sonko kuendelea kumkejeli Passairis katika mitandao ya kijamii licha ya kumkashifu wakati wa maadhimisho hayo ya kitaifa.

Kwa mujibu wa Kobia, wanawake wengi wanakabiliwa kwa kauli za kudhalilishwa mbele ya umma sawa na aliyoyapitia Passaris. Kobia amesema hali hiyo inashusha hadhi ya viongozi na hata wanawake katika jamii.

Amewashauri viongozi kuwa na hekima wakati wanapotoa hotuba zao kwa taifa na kwamba hakuna mtu yeyote, ikiwamo mwanamume au mwanamke anayependa kudhalilishwa mbele ya watu.

Amesema wizara yake itaendelea kushirikiana na washikadau mbalimbali ili kuhakikisha kuwa hakuna ukiukaji wa haki za kijinsia.

Ikumbukwe ni katika sherehe hiyo ambapo Sonko alimkemea vikali hatua ya Passaris kumpigia simu mara kwa mara, akisema kuwa yeye si mume wake ashike simu kila anapomtafuta baada ya Passari kudai huwa hapokei simu zake.

Related Topics