Raila akiri kusafiri kuelekea nchini Dubai

Sakata kuhusu biashara ya dhahabu bandia humu nchini imechukua mkondo mwingine huku Kinara wa Chama cha ODM, Raila Odinga akisema ndiye aliyefichua sakata hiyo. Raila amekiri kwamba alisafiri kuelekea nchini Dubai ili kuzungumza na mkuu wa milki za kiarabu, Sheikh Mohammed Bin Rahid Ali kuhusu suala hilo na kwamba alikuwapo wakati walaghai walipofanya mawasiliano ya simu ambayo yaliwahusisha viongozi mbalimbali.

Akizungumza katika halfa moja mjini Kisii, Raila amesema kwamba alimweleza Ali kuwa Waziri wa Masuala ya Ndani ya Nchi, Fred Matikang'i ambaye ni miongoni mwa waliotajwa kuwa ambao wangeweza kushinikiza kuachiliwa kwa dhahabu iliyonaswa asingeweza  kufanya hivyo na kwamba mazungumzo yaliyonaswa kuhusu uwezekano wa watu fulani serikali kushawishi kuachiliwa kwa dhahabu hiyo yalifanywa na walaghai.

Seneta Sam Ongeri aidha alizungumzia suala hilo huku akionekana kuwatetea waliohusishwa.

Ikumbukwe tayari maafisa wa Idara ya Upelelezi, DCI walithibitisha kwamba sauti iliyonaswa ilikuwa ya Seneta wa Bungoma Moses Wetangula ambapo alisikika akisema kuwa Rais Uhuru Kenyatta, Raila, vilevile Matiang'i watahakikisha dhahabu hiyo imeachiliwa.

Suala hilo liliibua hisia kali miongoni mwa wanasiasa huku Naibu wa Rais William Ruto akilitumia kuwasuta viongozi ambao wamekuwa wakimshtumu mara kwa mara kwa kumhusisha na ufisadi. Ruto aliwasuta viongozi waliohusishwa akisema hawafai kuchaguliwa na Wakenya kuhudumu katika nafasi zozote serikalini.

Related Topics

fake gold scandal