Daktari Hamisi Ali aliyeaga dunia nchini Cuba akiwa katika mafunzo yanayofadhiliwa na serikali ya Kenya atazikwa hapo kesho katika eneo la Shika Adabu, Likoni Kaunti ya Mombasa.
Katika taarifa rasmi, Wizara ya Afya hapo awali ilimesema Dkt. Hamisi aliaga dunia Jumapili tarehe 17 mwezi huu na chanzo cha kifo chake hakijabainika.
Taarifa zilibuka kuwa mwendazake ambaye ni Kakaye Mbunge wa Likoni Mishi Mboko alijiua, madai yanayopingwa na familia hiyo huku Kakaye Ali, Hamisi Juma Kurichwa akisema kuwa upasuaji wa kubaini kilichomuua utafanywa hapo kesho mwili ukiwasili kabla ya kuzikwa baada ya sala ya saa saba.
Dkt. Juma alikuwa miongoni mwa madaktari 50 ambao walikuwa wametumwa na Serikali ya Kitaifa nchini Cuba kupata mafunzo zaidi katika makubaliano baina ya mataifa haya mawili.