Sifuna amsuta Ruto kuhusu Mabwawa ya Aror na Kimwarer

Na Victor Mulama

Nairobi Kenya, Huku viongozi mbalimbali wakiendelea kumshinikiza Naibu wa Rais William Ruto kurekodi taarifa kuhusu anachojua kufuatia sakata ya mabwawa ya Aror na Kimwarer ambapo fedha takriban shilingi bilioni 21 zinadaiwa kufujwa, wa hivi punde amekuwa Katibu Mkuu wa Chama cha ODM, Edwin Sifuna.

Akihojiwa na idhaa ya hii, Sifuna amemsuta Ruto kwa kutoa ripoti ya jinsi fedha zilivyotumika kwenye miradi ya serikali ilhali Rais Uhuru Kenyatta alimtangaza Waziri wa Masuala ya Ndani ya Nchi, Fred Matiang'i kusimamia miradi ya serikali.

Wakati uo huo, Sifuna amesema ripoti ya Waziri wa Fedha, Henry Rotich inaonesha fedha zaidi ya shilingi bilioni 20 tayari zimelipwa kampuni ambazo zilijukumiwa kuendesha ujenzi wa mabwawa hayo ilhali Ruto anasema ni shilingi bilioni 7 pekee ambazo zinachunguzwa.

Ikumbukwe Mbunge wa Tiaty, William Kamket amemtaka Ruto kukoma kuzungumzia sakata hiyo kwenye mikutano ya hadhara. Akizungumza katika mtaa wa Akwichatis, Kamket amesema kauli zinazotolewa na viongozi mbalimbali kuhusu sakata ya ufujaji wa shilingi bilioni 21 zitakuwa muhimu iwapo viongozi hao watashirikiana na idara za uchunguzi. Aidha anasema serikali itahakikisha wahusika wanakabiliwa kwa mujibu wa sheria.

Related Topics