Aisha Jumwa atimuliwa rasmi ODM

Na Mate Tongola,

NAIROBI, KENYA, Hatimaye Mbunge wa Malindi Aisha Jumwa ametimuliwa rasmi kutoka chama cha ODM.

Baraza la Kitaifa la Chama cha ODM limeidhinisha pendekezo la Kamati ya nidhamu ya ODM ya kumtimua mbunge huyo kwa kukiuka sheria za chama hicho baada ya kuonekana hadharani akimpigia debe Naibu wa Rais William Ruto kuwania urais mwaka 2022.

Hata hivyo, hatma ya mwenzake wa Msambweni Suleiman Dori haijawekwa wazi kwani vilevile amekuwa akitangaza hadharani kumuunga mkono Ruto.

Mapema Ijumaa kinara wa chama hicho,  Raila Odinga, aliwaagiza wanachama wake kutilia mkazo sera za chama chao badala ya kukiuka sera zenyewe kwa misingi ya kuunga mkono ushirikiano wake na Rais Uhuru Kenyatta.

Akizungumza wakati wa mkutano wa Baraza Kuu la Chama hicho jijini Nairobi, Raila alisema ODM  hakitawaruhusu  wanachama wake kutumia ushirikiano huo katika kuhujumu shughuli za chama.

Ikumbukwe Jumwa na Dori walijipata matatani baada ya kutangaza kuunga mkono azimio la Naibu wa Rais, William Ruto kuwania urais mwaka wa 2022. Kamati ya Nidhamu ya ODM ilidai kuwa wawili hao walikiuka sheria za chama chao kwa kuunga mkono mgombea wa chama kingine kinyume na taratibu za sheria za vyama vya kiasiasa.

 

Hata hivyo wawili hao wamewasilisha malalmishi yao mahakamani ili kupinga hatua ya kufurushwa kwao wakisema nia yao ilikuwa kushirikiana na Naibu Rais William Ruto pamoja na kuendeleza umoja hasa kufuatia ushirikiano baina ya Rais na Raila maarufu Handshake.

Related Topics

aisha jumwa