Mwili wa mamaye mhubiri Pius Muiru wapatikana


Na Sofia Chinyezi
NAIROBI, KENYA, Mlinzi wa boma la mamaye mhubiri Pius Muiru, anazuiliwa baada ya kukiri kumuua mwanamke huyo. Maafisa wa upelelezi waliupata mwili wa Cecilia Wangari Mwangi siku moja baada ya kuripotiwa kutoweka, ukiwa umezikwa katika kaburi moja nyumbani kwake eneo la Murang'a. Mshukiwa ndiye aliyewaelekeza maafisa hao hadi eneo alikomzika.

Kamanda wa Polisi Kaunti ya Murang'a, Naomi Ichami anasema mlinzi huyo na mkaza-mwana wa Wangari wanazuiliwa, na kwamba wote watakaotajwa vilevile watahojiwa.

Mlinzi huyo alikamatwa baada ya kupatikana na simu ya marehemu ambayo aliitumia kujitumia shilingi tisini na tano katika simu yake. Inaarifiwa alifanya hivyo Jumanne jioni, saa ishirini na nne baada ya mwanamke huyo kutoweka.
Mwili wa mwendazake umelazwa katika hifadhi ya maiti baada ya kufukuliwa na maafisa wa polisi.