Serikali mekosa mwelekeo, vile vile na upinzani

Nchi yetu ya Kenya, tukufu ya kifahari

Likombolewa kwa damu Kenya,ya mababu hodari

Lipata uhuru Kenya, ila leo mna hatari

Amkeni ndugu wakenya, tuilinde nchi yetu

 

Maandamano kila kukicha, machafuko kila mahali

Ya taarifa video na picha, ya vifo vilivyotukabili

Majambazi usiku kucha, waua sawa na ajali

Amkeni ndugu wakenya, tuilinde nchi yetu

 

Serikali mekosa mwelekeo, vile vile na upinzani

Mauaji ovyo matokeo, maandamano ovyo mijini

Vitoa machozi matoleo, hamna utulivu nchini

Amkeni ndugu wakenya, tuilinde nchi yetu

 

Wanasiasa situtapeli, kutugawanya wananchi

Mezowea kutufeli, kutulaghai wenye nchi

Kwa vitendo kutukejeli, tulopiga kura wananchi

Amkeni ndugu wakenya, tuilinde nchi yetu

 

Wanasheria kule bungeni, mejaza sakata tele

Kuvua nguo humo bungeni, filimbi mayowe ndio ndwele

Mesahau sharia za nchini, kuzitunga tusonge mbele

Amkeni ndugu wakenya, tuilinde nchi yetu

 

Wito huu ni  mwamsho, sio wa vita bali Amani

Tusaidiane kufikisha mwisho, uhasama na chuki nchini

Na tufanye hamazisho, la umoja hapa nchini

Amkeni ndugu wakenya, tuilinde nchi yetu

 

Serikali na upinzani, zungumzeni kwa yakini

Tatueni shida kikaoni, sio kwa askari na mawe mijini

Mwapanda chuki mioyoni, mwa wafuasi wenu nchini

Amkeni ndugu wakenya, tuilinde nchi yetu

 

Tuungane sote pamoja, viongozi wananchi wote

Tutangamane kwa umoja, tupendane sisi sote

Tuzungumze lugha moja, ya Amani kote kote

Amkeni ndugu wakenya, tuilinde nchi yetu