;

Uchunguzi waendelea kuhusu Wakenya waliokwama Urusi

Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja akiwahutubia wanahabari jijini Mombasa Februari 27, 2026. [Robert Menza, Standard].

Inspekta Mkuu wa Polisi Douglas Kanja amesema serikali inaendelea na uchunguzi wa kina kuhusu ripoti za Wakenya wanaodaiwa kukwama nchini Urusi katika mazingira tata.

Kauli hiyo imetolewa huku kukiwa na ongezeko la malalamiko kutoka kwa familia zinazodai kuwa wapendwa wao walisafirishwa nje ya nchi kwa ahadi za ajira au fursa nyingine, lakini baadaye walijikuta katika hali ngumu isiyoeleweka.

Akizungumza jijini Mombasa, Kanja amewahakikishia Wakenya kuwa vyombo vya usalama vinafanya kazi kwa ushirikiano ili kubaini ukweli wa sakata hilo.

Amesema serikali haitasita kuwachukulia hatua kali za kisheria wote watakaobainika kuhusika na vitendo vyovyote vya ukiukaji wa sheria, ikiwemo ulaghai wa ajira au ulanguzi wa binadamu.

Kwa mujibu wa Inspekta Mkuu, uchunguzi huo unaongozwa na Idara ya Upelelezi (DCI), ambayo imepewa jukumu la kufuatilia kwa kina mtandao mzima wa waliohusika.

Maafisa wa idara hiyo wanachambua taarifa mbalimbali, ikiwa ni pamoja na nyaraka za usafiri, mikataba ya ajira na miamala ya kifedha, ili kubaini iwapo kulikuwa na ukiukaji wa sheria za ajira, ulanguzi wa binadamu au uhalifu mwingine wowote uliowezesha safari hizo.

Kanja amesisitiza kuwa serikali inalichukulia jambo hilo kwa uzito na kwa dharura, hasa kutokana na wasiwasi mkubwa uliotolewa na familia za watu wanaoripotiwa kukwama nje ya nchi.

Ameongeza kuwa mawasiliano yanaendelea kati ya mamlaka za Kenya na zile za Urusi ili kupata taarifa sahihi kuhusu hali ya Wakenya walioko huko na kuhakikisha haki zao zinalindwa.

Suala hilo limezua mjadala mpana kitaifa, huku baadhi ya wabunge na wanaharakati wakitaka kuwepo kwa mfumo thabiti zaidi wa kusimamia ajira za nje ya nchi.

Wamesema ni muhimu serikali kuimarisha ufuatiliaji wa mawakala wa ajira na kuhakikisha kuwa mikataba yote inafuata taratibu za kisheria kabla ya raia kusafiri.

Haya yanajiri wakati ambapo familia ya Erick Koome kutoka eneo la Kanyekine, Kaunti ya Meru, imeiomba serikali kuisaidia kufanikisha upatikanaji wa shilingi milioni 1.6 zinazodaiwa kukwama katika akaunti ya marehemu huyo katika benki moja ya Urusi.

Kwa mujibu wa familia, fedha hizo ni malipo aliyostahili Koome kabla ya kuuawa katika mapigano makali kati ya Urusi na Ukraine.

Familia hiyo imesema imekuwa ikikabiliwa na changamoto za kisheria na kiutaratibu katika kujaribu kupata fedha hizo, ikiwemo ukosefu wa nyaraka kamili na mawasiliano ya moja kwa moja na mamlaka husika za Urusi.

Wameitaka serikali ya Kenya kuingilia kati kupitia wizara zinazohusika na masuala ya nje ili kusaidia kufanikisha mchakato huo.

Wakati huo huo, Mahakama Kuu ya Kahawa imeagiza kuendelea kuzuiliwa kwa Festus Arasa Omwamba, ambaye amefikishwa mahakamani kwa tuhuma za kuhusika katika mtandao wa kusafirisha Wakenya kwenda Urusi kwa njia zisizo halali.

Omwamba anachunguzwa kuhusiana na madai ya ulanguzi wa binadamu na udanganyifu wa ajira, madai ambayo amekanusha.

Kwa mujibu wa mahakama, mshukiwa huyo atasalia rumande katika Kituo cha Polisi cha Kiambu hadi Machi 5, 2026, ambapo uamuzi utafanywa kuhusu iwapo ataachiliwa kwa dhamana au ataendelea kuzuiliwa wakati uchunguzi ukiendelea.

Upande wa mashtaka umeomba muda zaidi kukamilisha uchunguzi na kuwasilisha ushahidi wa ziada.

Kadiri uchunguzi unavyoendelea, macho ya wengi yameelekezwa kwa serikali kuona hatua zitakazochukuliwa ili kulinda raia wake na kuzuia matukio kama haya kujirudia siku zijazo.

.

RELATED NEWS