;

EU yatoa Euro milioni 63 kwa msaada wa dharura kwa walioathiriwa na njaa Somalia

(AP Photo/Farah Abdi Warsameh)

Umoja wa Ulaya umetangaza euro milioni 63, sawa na takriban shilingi bilioni 9.7, kwa ajili ya msaada wa kibinadamu kusaidia jamii zilizo katika mazingira magumu zaidi nchini Somalia.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, ufadhili huo unalenga watu walioathiriwa na migogoro ya muda mrefu, waliolazimika kuhama makazi yao, pamoja na athari za ukame mkali na kupanda kwa bei za chakula.

Takriban watu milioni 6.5, karibu theluthi moja ya raia wa Somalia, kwa sasa wanakabiliwa na njaa, huku watoto wapatao milioni 1.85 walio chini ya umri wa miaka mitano wakiwa katika hatari ya utapiamlo mkali.

Umoja wa Ulaya umesema msaada huo utaelekezwa katika huduma za afya na lishe zinazookoa maisha, ikiwemo matibabu ya utapiamlo mkali na wa papo hapo.

Fedha hizo pia zitatumika kwa msaada wa pesa taslimu wa dharura, huduma za maji safi na usafi wa mazingira, ulinzi kwa walio hatarini, pamoja na elimu ya dharura kwa watoto walioathiriwa na migogoro.

Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa, hali ya kibinadamu nchini Somalia inaendelea kuwa miongoni mwa ngumu zaidi duniani.

Migogoro ya ndani inayojirudia pamoja na mishtuko inayohusiana na mabadiliko ya hali ya anga imeendelea kuchochea uhamaji wa watu na kudhoofisha mafanikio ya maendeleo.

Maeneo yaliyoathiriwa zaidi ni pamoja na mikoa ya kati ya Galgaduud na Mudug, ambako karibu watu nusu milioni wameyakimbia makazi yao tangu Septemba mwaka jana.

Familia nyingi zinaendelea kuhama kutoka eneo moja hadi jingine kutafuta maji, malisho ya mifugo na chakula.

.

RELATED NEWS