;
Maafisa wa polisi katika eneo la Athi River, Kaunti ya Machakos, wamefanikiwa kukamata washukiwa wawili wanaoaminika kuwa wanachama wa genge lenye vijana 15 linalojihusisha na wizi na uhalifu wa mara kwa mara katika eneo hilo na maeneo jirani.
Akithibitisha tukio hilo, Afisa Mkuu wa Makachero wa DCI tawi la Athi River, Michael Boiyo, alisema washukiwa hao ni Brian Mutuku maarufu Brayo na Ephantus Karanja, ambao ni miongoni mwa vijana wa genge hilo linalosababisha hofu kwa wakazi wa Athi River.
Boiyo alisema kukamatwa kwao kulijiri baada ya polisi kupata taarifa kuhusu kundi la vijana ambalo lilivamia na kuibia wafanyabiashara katika mtaa wa Makadara, eneo la Athi River. Polisi walifanya opareheni kali na hatimaye wakafanikiwa kuwakamata washukiwa wawili.
Polisi walikabiliwa na changamoto wakati genge hilo lilijaribu kuwafurusha kwa kuwatupia mawe, jambo lililowalazimu polisi kufyatua risasi hewani ili kulitawanya kundi hilo. Baadaye, baada ya mbio za paka na panya, washukiwa wawili walipatikana na bastola moja ghushi, kisu, panga na misokoto 19 ya bangi.
Afisa huyo alibainisha kuwa Brian Mutuku, maarufu Brayo, anakabiliwa na kesi nyingine kadhaa zinazohusiana na visa vya uhalifu katika eneo hilo, ambazo zinaendelea mahakamani.
Polisi sasa wanawaomba wananchi, hasa wamiliki wa biashara waliopata hasara kutokana na tukio hilo, kuandikisha ripoti zao katika Kituo cha Polisi cha Athi River. Aidha, Boiyo ameitaka jamii kutoa taarifa yoyote kuhusu genge hilo, akihakikishia kuwa ripoti zote zitashughulikiwa kwa siri.
Hii ni sehemu ya juhudi za polisi kudhibiti uhalifu na kuimarisha usalama wa wakazi wa Athi River, huku wakitilia mkazo ushirikiano wa jamii katika kutoa taarifa muhimu za kiusalama. Tukio hili linaonyesha jinsi operesheni za polisi zinavyoweza kudhibiti genge, lakini pia limeibua umuhimu wa wananchi kushirikiana na vyombo vya sheria ili kuzuia uhalifu na kulinda mali yao.