;

Vifo vya akina mama vyapungua kwa asilimia 34 Kisii

Mkurugenzi Mtendaji Mwenza wa Jacaranda Health, Cynthia Kahumbura. [Robert Menza, Standard]

Vifo vya akina mama wajawazito vimepungua kwa kiasi kikubwa katika Kaunti ya Kisii, kufuatia utekelezaji wa mpango wa kuimarisha mfumo wa afya katika kaunti za Mombasa, Kisii na Makueni.

Data mpya inaonesha kuwa vifo vya akina mama katika Kaunti ya Kisii vimepungua kwa asilimia 34.5 ndani ya kipindi cha miaka mitatu iliyopita, kutoka vifo 159 hadi 104 kwa kila vizazi 100,000 vilivyo hai.

Mafanikio haya yanahusishwa na maboresho katika huduma za dharura za uzazi pamoja na matumizi ya zana za kidijitali katika sekta ya afya.

Matokeo hayo yanatokana na utekelezaji wa mradi wa Kenya Quality Ecosystem, au KQE, ambao unalenga kubadilisha data ya kawaida ya afya kuwa hatua za haraka za kimatibabu. Mradi huo ulianzishwa mwaka 2023 kwa lengo la kuboresha matokeo kwa akina mama wajawazito na watoto wachanga.

Mpango huo ni ushirikiano kati ya shirika la Jacaranda Health, linalojitolea kuboresha afya ya mama na mtoto, Health Systems Insight, pamoja na serikali za kaunti za Mombasa, Kisii na Makueni.

Mbali na kuimarisha mifumo ya data, mpango huo pia unajumuisha ushauri kwa wahudumu wa afya walioko mstari wa mbele pamoja na usaidizi wa kifedha ili kuboresha utoaji wa huduma.

Akizungumza jijini Mombasa wakati wa mkutano wa mabadilishano ya uzoefu kati ya kaunti hizo, Mkurugenzi Mtendaji Mwenza wa Jacaranda Health, Cynthia Kahumbura, ameisitiza umuhimu wa kuunganisha na kutumia data ipasavyo katika mifumo ya afya ya umma ili kuokoa maisha zaidi.

.

RELATED NEWS