;
Mgawanyiko ndani ya chama cha ODM unaibuka wazi.
Tawi la Linda Mwananchi linafanya kazi dhidi ya uongozi wa Oburu Odinga, likipinga mkataba wa makubaliano na UDA na kudai demokrasia ndani ya chama kupitia NDC.
Viongozi hao wanasisitiza kuwa ODM inapaswa kubaki chama cha kitaifa, kuendeleza ajenda ya kisiasa ya Raila Odinga, na kuhakikisha kuwa uongozi unaonesha kizazi kipya, kisasa na cha maendeleo badala ya uteuzi wa kisiasa unaotokana na haraka au kuimarisha muungano wa kisiasa wa dharura.
Kundi la Linda Mwananchi linaongozwa na Katibu Mkuu wa ODM, Edwin Sifuna, Gavana wa Siaya James Orengo, Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi, na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino.
Linda Mwananchi ni tawi la waasi wa ODM linalopingana na mpango wa mkataba unaopendekezwa na chama na UDA, chini ya Rais William Rutokama ilivyopendekezwa na Kamati Kuu ya Usimamizi (CMC) ya ODM. Kamati hiyo ilimtaka kiongozi wa chama, Oburu Odinga, kuanzisha mazungumzo ya awali ya muungano na UDA, kama sehemu ya mkakati wa chama katika kujiandaa kisiasa kabla ya uchaguzi mkuu.
Hata hivyo, kundi hili la Linda Mwananchi limejitenga na tawi kuu la ODM linaloongozwa na Oburu Odinga, ambalo limekuwa likiendesha mikutano ya chama inayoitwa ODM Linda Ground, inayolenga kukusanya maoni ya wanachama kote nchini juu ya iwapo chama cha Orange kinapaswa kuingia katika muungano wa kisiasa na UDA.
Mikutano ya Linda Ground imepokelewa na ukosoaji mkali kutoka kwa Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna, ambaye amehoji chanzo cha ufadhili wake. Sifuna anasema mikutano hiyo inafadhiliwa kutoka nje ya chama na si kutoka hazina za ODM, akibainisha kuwa fedha za chama zilitumika mara ya mwisho wakati wa sherehe ya maadhimisho ya miaka 20 ya ODM.
“Mikutano inayojulikana kama Linda Ground haifadhiliwi na chama. Mara ya mwisho fedha zilitolewa kutoka akaunti za ODM ilikuwa wakati wa maadhimisho ya ODM at 20 iliyofanyika Mombasa. Wakenya wanastahili kujua nani anayefadhili mikutano hii,” alisema Sifuna.
Tawi la Linda Mwananchi lilianzia mikutano yake kanisani Kangemi, Nairobi, ambapo wanachama walitumia fursa hiyo kushiriki mapigano ya kisiasa dhidi ya viongozi wa tawi la Linda Ground linaloongozwa na Oburu, na waliokuwa wakifanya mkutano huo kwa wakati mmoja Kisii.
Sehemu ya viongozi wa Linda Mwananchi pia wanapinga uongozi wa Oburu Odinga. Mbunge wa Embakasi Mashariki, Babu Owino, amekuwa akitaka kuondolewa kwa Oburu, akisisitiza kuwa uongozi wa chama unapaswa kuchaguliwa kupitia Mkutano wa Kitaifa wa Wawakilishi (NDC).
“ODM lazima iendeshwe kwa mapenzi ya wanachama wake, si kwa uteuzi. Kiongozi wa chama anaweza kuchaguliwa tu kupitia NDC, na hiyo ndiyo tunayoitaka,” alisema Babu.
Babu amesisitiza kuwa yeye ndiye anastahili kuwa kiongozi wa chama, si Oburu, na amedai mkutano wa NDC ufanyike haraka ili kutatua mgogoro huu. Amesema kuwa baada ya kifo cha aliyekuwa kinara wa ODM Raila Odinga, uongozi ungepaswa kuhamia kwa kizazi kipya.
“Baada ya kifo cha Raila Odinga, uongozi ungepaswa kuhamia kizazi kipya. Kama Musa alivyomkabidhi Joshua badala ya Aaron, ODM inahitaji uongozi mchanga, wa kisasa na wa maendeleo.”
Mbunge wa Saboti, Caleb Amisi, pia amepinga uteuzi wa Oburu Odinga kama kiongozi wa chama, akieleza kuwa ni kinyume cha katiba. Amisi anasema katiba ya ODM inaeleza kuwa kiongozi wa chama anaweza kuchaguliwa tu kupitia NDC, na uteuzi wowote mwingine ni haramu.
Gavana wa Siaya, James Orengo, ambaye amekuwa mstari wa mbele kupinga mkataba wowote na UDA, ametahadharisha kuwa ODM ina hatari ya kupoteza tabia yake ya kitaifa. Amesema chama, kilichopo kwa zaidi ya miaka 20, kinaweza kupunguzwa kuwa chama cha kikanda au cha Kabila fulani, na kupoteza mtazamo wa kitaifa.
“ODM ilijengwa kama chama cha kitaifa, si kikanda au cha kikabila. Kuingia kwenye mkataba wa haraka kunaweza kupunguza chama kuwa chama la Luo na kufutwa tabia ya kitaifa ambayo Raila Odinga alijenga kwa miaka 20. Hatuwezi kuacha misingi yetu na historia kwa urahisi wa kisiasa,” alisema Orengo.
Mintarafu ya hayo, Seneta wa Vihiga, Godfrey Osotsi, pia amepinga haraka ya chama kuingia katika muungano na UDA. Amesema ODM inapaswa kuendeleza ajenda ya pointi 10 ambayo Raila Odinga alikuwa nayo na ambayo pia ilitolewa kama msingi wa makubaliano yake na Rais William Ruto.