;
Jeshi la Kitaifa la Somalia (SNAF), likishirikiana na wanajeshi wa Uganda chini ya Ujumbe wa Umoja wa Afrika nchini Somalia (AMISOM) na washirika wa kimataifa, limeanzisha operesheni mpya katika eneo la Lower Shabelle, kusini mwa Somalia, ikilenga wanamgambo wa Al-Shabaab.
Kwa mujibu wa Wizara ya Ulinzi ya Somalia, operesheni hiyo iliyopewa jina la “Rolling Thunder” inalenga kubomoa ngome kuu za kundi hilo, kuvuruga njia zinazotumika kupanga na kutekeleza mashambulizi, pamoja na kulinda raia na maeneo muhimu ya kilimo.
Katika taarifa, Wizara hiyo imesema operesheni itaendelea hadi Al-Shabaab itakapoondolewa kabisa kama tishio kwa amani, maendeleo na ujenzi wa taifa.
Serikali imeeleza kuwa wanajeshi wake wanaendelea na operesheni hiyo hata katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadhani, ikisisitiza dhamira ya vikosi vya usalama katika kurejesha utulivu.
Operesheni hiyo inafanyika wakati Somalia imeongeza mashambulizi dhidi ya kundi hilo katika miezi ya karibuni, hatua inayosemekana kupunguza idadi ya wanamgambo na uwezo wao wa kushambulia.
Mapema mwezi huu, mamlaka zilitangaza kuuawa kwa kamanda mkuu wa Al-Shabaab, Ahmed Dhubad Xidig, anayejulikana pia kama Sheikh Adan Dheere.
Kwa mujibu wa Shirika la Ujasusi na Usalama la Kitaifa (NISA), kamanda huyo aliuawa Januari 27 katika operesheni maalum iliyofanywa na Kikosi cha Gaashan eneo la Daniga Baalow, Lower Shabelle, baada ya kupinga vikosi vya usalama wakati wa uvamizi.
NISA ilisema Ahmed, aliyejiunga na Al-Shabaab mwaka 2008, alikuwa akisimamia fedha za kundi hilo katika eneo la Banadir na aliwahi kuhusika katika shughuli za unyang’anyi katika mikoa ya Mudug, Galgaduud, Hiran na Lower Shabelle.
Kifo chake kilitangazwa siku chache baada ya vikosi vya usalama kumuua mkuu mwingine wa fedha wa kundi hilo, Abdullahi Hassan Abdi Osoble, katika operesheni tofauti.
Al-Shabaab imekuwa ikidhibiti sehemu za kusini mwa Somalia kwa miaka kadhaa, ikitumia maeneo hayo kama vituo vya kupanga mashambulizi na kuendesha biashara haramu, ikiwemo ulanguzi wa binadamu.